Home Uncategorized BALINYA: OKWI AMENILETA YANGA

BALINYA: OKWI AMENILETA YANGA


MSHAMBULIAJI mpya wa Yanga, Juma Balinya raia wa Uganda amefunguka kwamba moja ya watu ambao wamechangia yeye kutua Yanga ni mshambuliaji wa Simba, Emmanuel Okwi.

Balinya aliyekuwa akiwaniwa na Simba juzi Jumamosi alitambulishwa Yanga baada ya kumalizana na mabosi wa timu hiyo chini ya mwenyekiti wake, Dk Mshindo Msolla. Balinya ndiye mfungaji bora wa Ligi Kuu ya Uganda kwa msimu uliopita akifunga mabao 19.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Balinya amemtaja Okwi kuwa mmoja wa watu ambao ni marafiki zake ambao wamemshawishi yeye kuja kucheza Ligi Kuu ya Tanzania Bara.

Pia straika huyo ameongeza kwamba kwenye suala la kutupia mabao mashabiki wa timu hiyo wasijali kutokana na ndiyo kazi yake ambayo imemfanya asajiliwe klabuni hapo.

“Yanga hapa sikuwa namjua mtu kabla ya kusaini mkataba lakini marafiki zangu ni Okwi (Emmanuel) na Juuko Murshid ambao nilikuwa ninawasiliana nao.

“Lakini hao ndiyo pia wamenifanya nije hapa Tanzania kucheza mpira kutokana na kile ambacho walikuwa wananiambia.

“Kuhusu suala la mimi kufunga, hilo ndiyo jukumu langu hadi viongozi kuja kunisajili, wasijali kuhusiana na hilo kwani nimejipanga na nitafunga mabao kwa kadiri nitakavyoweza,” alisema Balinya.

SOMA NA HII  KMC WAMALIZANA NA MAJEMBE MAWILI YA CONGO