Home Uncategorized MAN UNITED YANASA BONGE LA BEKI

MAN UNITED YANASA BONGE LA BEKI


MANCHESTER UNITED ipo kwenye hatua za mwisho za kukamilisha usajili wa beki Aaron Wan-Bissaka. Wan-Bissaka anatajwa kama miongoni mwa mabeki bora wa pembeni kwenye Ligi Kuu England.

Klabu hiyo imefikia muafaka wa kulipa ada ya pauni milioni 50 (Sh. bilioni 146) ili kumsajili beki huyo wa pembeni wa Crystal Palace. Pamoja na ada hiyo, pia Wan-Bissaka ameahidiwa mshahara mnono na Manchester United.

Wan-Bissaka anayelipwa kwa sasa mshahara wa pauni 10,000 (Sh. milioni 29) kwa wiki, ameahidiwa kupata kitita cha pauni 80,000 (Sh. milioni 233) kwa wiki katika klabu yake mpya wa Manchester United. Beki huyo anatazamiwa kwenda Manchester kufanyiwa vipimo kabla ya kukamilisha taratibu za usajili.

Wan-Bissaka atakuwa mchezaji wa pili kusajiliwa na kocha wa Manchester United, Ole Gunnar Solskjaer baada ya kumpata kiungo Dan James aliyekuwa Swansea City. Mkurugenzi wa Ufundi wa Palace, Dougie Freedman ndio alikutana na viongozi wa Manchester United kukamilisha dili hilo.

Freedman alikuwa Italia ambako alikuwa anafuatilia michuano ya soka ya Ulaya ya vijana wenye umri wa chini ya 21 ambako Wan-Bissaka alikuwemo katika kikosi cha England kilichotolewa kwenye makundi.

Mara ya kwanza Manchester United ilitaka kutoa dau la pauni milioni 35 (Sh. bilioni 102) lakini lilikataliwa na Crystal Palace. Solskjaer atakuwa amefurahishwa na kumpata Wan-Bissaka kwani atacheza kama beki wa kulia kwani kwa sasa walikuwa wanamtegemea zaidi mkongwe Ashley Young.

SOMA NA HII  AHUKUMIWA KUSAFISHA HOSPITALI MIEZI 12 KWA KUMUUA MKEWE