Home Uncategorized MNYARWANDA WA YANGA ATIMKIA ZAMBIA

MNYARWANDA WA YANGA ATIMKIA ZAMBIA


KAMA Yanga hawatakaza uzi vizuri basi wapo mbioni kumkosa beki Mnyarwanda, Eric Rutanga ambaye wamekuwa wakimpigia hesabu kwa kiasi kikubwa kutokana na beki huyo kuwa njiani kutua Nkana FC ya Zambia.

Rutanga ambaye anacheza nafasi ya beki wa kushoto, ni mmoja wa wachezaji ambao kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera anayetaka asajiliwe na mabosi wa timu hiyo kwa msimu ujao.

Rutanga anayeichezea Rayon Sports, anatakiwa na Yanga kwa ajili ya kuongeza nguvu upande wa beki ya kushoto ambapo wapo Gadiel Michael aliyemaliza mkataba na Mwinyi Haji ambaye anaweza kuachwa.

Habari za uhakika ambazo Championi Jumatano, limezipata ni kwamba beki huyo anaweza kujiunga na Nkana ya Zambia baada ya kuona dili lake kwenda Yanga likiwa halina uhakika.

“Ni kweli kwa sasa Nkana wamekuja kumtaka Rutanga na hali inavyoonekana anaweza kwenda huko kutokana na dili la kwenda Yanga kusitasita.

“Awali walikuwa siriazi na ikaonekana anaenda huko lakini kwa sasa wamepunguza, hivyo beki huyo ameamua kwenda Nkana ambapo wameonyesha nia ya kumtaka,” kilisema chanzo hicho.

Alipotafutwa Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Fredrick Mwakalebela kuhusiana na hilo, alisema: “Tulishamaliza usajili wa kimataifa na ndiyo maana sasa unaona wachezaji tunaosajili ni wa ndani tu. Lakini kama itatokea mwalimu Zahera atasema tumsajili basi tutamsajili kwani hatushindwi kumsajili mchezaji yeyote yule.”

SOMA NA HII  YANGA WATAJA SABABU YA KUCHEZA MECHI ZA KIRAFIKI