Home Uncategorized ALIYEELEZWA KUHITAJIKA YANGA APIGWA CHINI KENYA

ALIYEELEZWA KUHITAJIKA YANGA APIGWA CHINI KENYA


KOCHA wa Bandari FC inayoshiriki Ligi Kuu ya Kenya, Bernard Mwalala ameondoka katika klabu hiyo baada ya matokeo mabaya kufuatia kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Tusker juzi Jumapili kwenye Uwanja wa Mbaraki Sports hapa, imeelezwa.

Mwalala alijiunga na klabu hiyo mwaka 2018 akitokea Nzoia Sugar na kuiongoza hadi kucheza mashindano ya kimataifa baada ya kushinda taji la nyumbani msimu uliopita, lakini klabu hiyo imechemsha msimu huu.

Bandari kimsimamo iko katika nafasi ya 11 ikiwa na pointi 18 baada ya kushuka dimbani mara 16. Kulikuwa na mijada kuwa hatma ya Mwalala ilikuwa hatarini, huku chanzo cha uhakika kilisema kuwa kocha huyo hatmaye aliamua kuachana na klabu hiyo baada ya Bandari kufungwa na Tusker juzi.

“Kocha ameombwa kuachia ngazi na klabu itatangaza rasmi kesho (juzi Jumatatu), “chanzo hicho kilisema juzi Jumapili. Kocha wazamani wa timu ya taifa ya Kenya, Harambee Stars, Twahir Muhiddin amekuwa akihusishwa na kibarua hicho kama kocha wa muda ili kuinusuru meli hiyo inayotaka kuzama.

Katika mchezo huo wa juzi, bao la dakika za mwisho lililofungwa na Brian Marita liliiwezesha Tusker kuifunga Bandari 2-1 katika mchezo mkali wa Ligi Kuu ya Kenya uliofanyika kwenye Uwanja wa Mbaraki Sports Club hapa.

Bandari ilianza mchezo huo vizuri na ndio ilikuwa ya kwanza kupata bao katika kipindi cha kwanza kupitia kwa Wycliffe Ochomo, kabla Tusker kufanikiwa kusawazisha kupitia kwa Hashim Sempala.

Mwalala wakati wa uchezaji wake aliwahi kuwika na Yanga ya Tanzania na kucheza nayo hadi michuano ya Ligi ya Mabingwa wa Afrika msimu wa mwaka 2006 na 2007 baada ya kuichezea Club Sports Villa ya Uganda msimu wa 2004/05.
SOMA NA HII  DK MSOLLA "AITUMBUA" KAMATI YANGA, AUNDA KAMATI MPYA YA MASHINDA, MAJINA HAYA HAPA...