Home Uncategorized MARIOO, UJUMBE WAKO HUU HAPA ULIACHWA NA MRESSY

MARIOO, UJUMBE WAKO HUU HAPA ULIACHWA NA MRESSY


MCHAKAMCHAKA mkubwa wa maisha ni kila siku mchana hata usiku lengo kubwa ikiwa ni kutafuta riziki kwa namna ambayo Mungu anajaalia.
Wapo wengine ambao wanapambana kupata riziki kupitia muziki wakiandika na kuandikiwa nyimbo mwisho wa siku mkono unaenda kinywani.
Yote kwa yote wapo wasanii ambao wanapiga hatua kubwa na kufikia kuwa wasanii wa kimataifa na wanatangaza nchi kwa upana na wapo ambao kila siku wapo vilevile kutokana na chaguo la maisha ambayo wameamua kuyafanya.
Leo nipo na Marioo, msanii wa muziki wa kizazi kipya ambaye anafanya kazi yake vizuri kwenye anga la muziki kwa sasa na wengi wanamkubali kutokana na kipaji chake.
Msikilize kwenye inatosha nadhani utaelewa kwamba ana kitu anaweza kukiandika na kuimba pia kwa sauti nzuri na inayovutia.
Kwa sasa ngoma yake mpya ni Unanionea inafanya poa pia kwenye vituo vya redio huyu ni Marioo, jina lake halisi anaitwa Omary Mwanga.
Chibonge ilikuwa  ni ngoma kali pia ila kwangu mimi hata wewe pia Dar Kugumu iliyoachiwa Februari 23 kwenye mtandao wa You Tube ilikuwa inakuvutia.


Julai 10, unatimiza mwaka mmoja ukiwa umetuacha. Ilikuwa ngumu kuamini ila ni kazi ya Mungu haina makosa ndugu yangu hivyo leo naandika ule ujumbe ambao uliniachia niupeleka kwa Marioo.
Sikuandika kwa muda kwa kuwa bado nilikuwa namsikiliza nimuelewe kuna nini kwenye utunzi wake naona bado anapambana kufikia malengo yake.
Marioo ujumbe wako ambao ndugu yetu Ibrahim Mressy aliniachia  enzi za uhai wake ni kwamba anakuona unakuja vizuri kwenye muziki na alikuweka kwenye daraja la Ali kiba, Diamond na Harmonize.
Alikuambia kwamba kwa namna ambavyo unajituma ikiwa utakuwa katika ubora wako na hautakuwa na dharau itakuwa rahisi sana kwako kufiki ndoto zako.
Jambo la msingi ambalo aliniambia ni kwamba unahitaji kuwa makini kwa marafiki zako pamoja na kufanya kazi kwa umakini kwani wengi wanakuamini na kukufuatilia pia.
Mressy eh, ni ngumu kuamini kwamba umeondoka lakini upendo wako unaishi ndani ya Global Group na wafanyakazi wote.
Achana na wafanyakazi hata wale ambao wanatuzunguka pia bado unaishi ndani ya mioyo yao, hakuna mwingine amefikia ile hatua ya kujitoa kwa ajili ya wengine.
Nakumbuka namna tulivyokuwa tukienda kazini pamoja na kwenye gazeti hili ile kazi yangu ya kwanza ilitoka . 
Tuliandika  pamoja baada ya kutoka pale makao makuu ya Shirikisho la Soka Tanzania,(TFF).
Ulikuwa hupendi kuona gazeti linatoka bila kazi yangu kuwepo ‘Clean sheet’ nakumbuka wakati mwingine ukiona nimekwama  ulikuwa unaniita na tunafanya kazi kwa pamoja na nikikuzingua unacheka bila kukasirika na maisha yanaendelea.
Brother pumzika kwa amani.Ujumbe ulioniachia kwa ajili ya Marioo nimeufikisha ndugu yangu, sina deni kwa Marioo ni kazi kwake kutimiza ulichomwambia.
 Pia nakukumbusha kuwa sheet zinatoka kama kawaida.

Ujumbe huu aliachiwa Lunyamadzo Mlyuka aliyekuwa rafiki wa karibu wa Mressy ndani ya Global Group.
SOMA NA HII  CHEKI MOTO WA KIKOSI BORA CHA MSIMU WA 2019/20