Home Uncategorized KABLA YA KUMWAGA WINO MCHEZAJI ITAPENDEZA UKIUELEWA MKATABA

KABLA YA KUMWAGA WINO MCHEZAJI ITAPENDEZA UKIUELEWA MKATABA

 WIMBO unaoimbwa kwa sasa kila kona ni masuala ya usajili ambapo kila timu inapambana kuboresha kikosi chake ili kiwe cha ushindani  msimu wa 2020/21.

 

Kwa namna ambavyo wanaona wao ndivyo ambavyo wanafanya kwenye maboresho kwenye timu zao hasa katika sehemu ambazo hawajafanya vizuri kwa msimu wa 2019/20.

 

Milango ilikuwa wazi kuanzia Agosti Mosi kisha inatarajiwa kufungwa Agosti 31 kwenye masuala ya usajili muhimu kila timu ikazingatia wakati kwani ni jambo la msingi kwenye kuyakimbizia mafanikio.

 

Tayari Azam FC, Yanga na Simba nao wameonekana kuingia kazini bila kuwasahau Namungo. Gwambina FC pamoja na Dodoma hizi mbili zimepanda Ligi Kuu Bara msimu huu.

 

Wakati ambao wachezaji wanakuwa bize kusaka timu na kuingia kwenye kazi mpya ni sasa hivyo nao pia wanapaswa wawe makini katika kila hatua ambazo wanapitia.

 

Ipo wazi kwamba kuna wengine walishindwa kuonyesha makubwa ndani ya msimu uliopita mkono wa kwa heri unawahusu huku wengine wakishindwana kwenye masuala ya maslahi.

 

Kinachotakiwa kwa sasa kila mmoja kuangalia namna gani anapata kile ambacho anakihitaji kwa kuzingatia maslahi yake pamoja na mkataba unamueleza nini.

 

Wachezaji wetu wengi tunakwenda kwa kubahatisha hasa tukiwa hatuna ile mipango makini kwa ajili ya kesho jambo ambalo limekuwa likileta matatizo hapo baadaye.

 

Kwa wale ambao walishawahi kukosea wakati uliopita kwenye upande wa mkataba basi muda huu ni kuangalia namna gani wanaweza kurekebisha kwa kuangalia upya namna ya kuingia kwenye makubaliano.

 

Jambo la msingi kabla ya kusaini inapendeza mchezaji auelewe mkataba unataka nini na yeye anahitaji nini jambo ambalo litasaidia kuweza kuwa katika mpangilio mzuri.

 

Ikiwa mchezaji atasaini mkataba bila kuelewa vizuri utamletea matatizo hapo baadaye hivyo jambo la msingi ni kuusoma na kuelewa unataka nini mkataba na yeye anahitaji nini.

 

Pia itapendeza wakati wa kusaini mikataba kwa sasa wachezaji wakapata ushauri kutoka kwa wataalamu wa masuala ya sheria kwa kuwa mkataba ni mahesabu yanachezwa ukiingia bila kujua utakuja kujuta baadaye.

SOMA NA HII  YANGA YAGAWANA POINTI MOJAMOJA NA AZAM FC, MABAO MAWILI YA AZAM YAMEYEYUKA MAZIMA

Ikitokea umeanza maisha mapya ni lazima uishi kwa kuzingatia utaratibu ambao umepewa itasaidia kutokuwa na matatizo ya mara kwa mara na timu yako ambayo utakuwa umeingia nayo kwenye makubaliano.

 

Timu pia ziwe wazi kwa wachezaji ambao muda wao umekwisha na hawana hesabu za kuwaongezea mkataba ili kufungua njia kwa wengine wanaosubiri wachezaji huru kuwachukua.

 

Usajili una mambo mengi ila kwa sasa muda unazidi kukimbia hivyo ni muhimu kwa kila timu na wachezaji kupambana kupata nafasi kule ambako wanatakiwa kwenda.

 

Wachezaji ambao walishindwa kufanya vizuri kwa msimu wa 2019/20 ninajua kwa sasa wanapambana kupata sehemu ya kucheza ikitokea wakapata timu basi waache ile jeuri ambayo walikuwa nayo mpaka wakashindwa kuonyesha uwezo lakini wanatakiwa kuuelewa mkataba kabla ya kusaini.