Home Uncategorized LUSAJO MTAMBO WA MABAO NDANI YA NAMUNGO UNAOHUSISHWA KUJIUNGA YANGA

LUSAJO MTAMBO WA MABAO NDANI YA NAMUNGO UNAOHUSISHWA KUJIUNGA YANGA

 

UKIWATAJA wazawa wakali wa kucheka na nyavu kwa msimu wa 2019/20 walio ndani ya tano bora, huwezi kuliacha jina la Reliants Lusajo anayekipiga ndani ya Namungo.

Nyota huyo amekuwa na mwendelezo wa kucheka na nyavu kwa misimu miwili mfululizo akiwa ni namba moja ndani ya kikosi cha Namungo FC kinachonolewa na Hitimana Thierry.

 

Kwa msimu wa 2019/20, wazawa walio ndani ya tano bora wanaongozwa na Yusuph Mhilu wa Kagera Sugar na Wazir Junior wa Mbao wenye mabao 13, huku Lusajo, Peter Mapunda wakiwa na mabao 12 kila mmoja.


Msimu wa 2018/19 akiwa Namungo wakati huo inashiriki Ligi Daraja la Kwanza, alitupia mabao 15 na kuwa mfungaji bora na msimu wa 2019/20 ndani ya Ligi Kuu Bara, ametupia jumla ya mabao 12, hivyo kwa misimu miwili mfululizo Lusajo kibindoni ana mabao 27.

 

Kwa sasa anatajwa kuingia rada za Yanga inayoboresha kikosi chake wakiwa tayari wameshamalizana na nyota wazawa ikiwa ni pamoja na Wazir Junior aliyekuwa mshambuliaji wa Mbao, Bakari Mwamnyeto aliyekuwa Coastal Union, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ aliyekuwa akikipiga MFK Vyskov ya Jamhuri ya Czech, Kibwana Shomari aliyekuwa Mtibwa Sugar. na Yassin Mustapha hawa ni mabeki, na kiungo Zawadi Mauya aliyekuwa Kagera Sugar na Farid Mussa, huru.

 

Inaelezwa kuwa baada ya kumalizana na hao wote, anayefuata kupewa dili la Yanga ni Lusajo aliyewahi kukipiga ndani ya kikosi hicho kwa msimu wa 2013 ila alikosa namba kikosi cha kwanza.

 

Huyu hapa Lusajo anazungumza kuhusu mkataba wake na atakakoibukia msimu wa 2020/21:-


“Ninamshukuru Mungu, tumemaliza msimu wa 2019/20 salama kwa kuwa tumefika kwenye malengo yetu ya kumaliza ndani ya tano bora pamoja na kucheza fainali ya Kombe la Shirikisho.

 

UNADHANI KIPI KILIIBEBA NAMUNGO?

“Kila mchezaji alikuwa na utayari katika kazi kwa pamoja na malengo ambayo tulikuwa tumejiwekea, tulipambana kuweza kuyafikia ndiyo maana tumeweza kufanikiwa.


MABAO 12 KWA MSIMU ULISTAHILI KUWA NAYO?

SOMA NA HII  MZUNGUKO WA PILI MTIBWA SUGAR YAPANIA KUFANYA VIZURI

“Kwa kiasi fulani nilistahili kwa kuwa nayo ndiyo ambayo nipo nayo kwa sasa lakini ninaamini kwamba ningekuwa fiti muda wote ningefunga zaidi ya hayo ila kwa kuwa nipo nayo kwa sasa ni wakati wangu wa kujipanga kwa wakati ujao.


MSIMU UJAO UTAKUWA WAPI?

“Bado sijajua kwa sasa kwa kuwa tulipomaliza mchezo wetu dhidi ya Simba, nilipewa likizo na nipo mapumziko kwa sasa, hivyo mambo yakiwa sawa nitajua wapi nitakuwa ila masuala yote yapo kwa meneja wangu.


MKATABA WAKO NAMUNGO UPOJE?

“Mkataba wangu umeshaisha kwa sasa sijaongeza mkataba mwingine ndani ya Namungo.


UNATAJWA KUIBUKIA YANGA HILI UNALIZU NGUMZIAJE?

“Kwangu mimi sina tatizo kwani ukiwa mchezaji huwezi kuchagua kambi, kwangu ni biashara, ninasaini bila tatizo ndani ya Yanga hata Ndanda wakija sina tatizo nao ila kikubwa ni maslahi ya pale ambapo ninakwenda kucheza.


ULISHAWAHI KUCHEZA YANGA UKAKWAMA, UNADHANI UTAWEZA KUTUSUA UKIRUDI?

“Tatizo la awali sikuwa ninacheza kikosi cha kwanza, pia masuala ya masomo yalikuwa yananibana ila kwa kuwa nimewekeza kwenye michezo jumla sifikirii kufeli nikipata nafasi tena pale, uwezo ninao, kikubwa wafuate utaratibu mimi sina tatizo,” alimaliza Lusajo.

Championi Jumatatu lilimtafuta meneja wa Lusajo, Ahmed Omary maarufu kama Presidaa alisema kuwa mteja wake yupo huru baada ya kumalizana na Namungo.

“Lusajo yupo huru kwa kuwa mkataba wake na Namungo umekwisha, jambo la kwanza tumeipa Namungo nafasi kusikiliza ofa yao kisha hizi nyingine ambazo zinakuja zitafuata, kuna ofa nyingi ambazo zimekuja mkononi kwa sasa hivyo timu zote hata ikiwa Yanga, Azam FC ikiwa zinamhitaji ni suala la kukaa mezani,” alisema.