Home Uncategorized NYOTA WA BRAZIL AMPA TANO BWALYA

NYOTA WA BRAZIL AMPA TANO BWALYA


KIUNGO wa Simba, Gerson Fraga Vieira raia wa Brazil amesema kuwa usajili wa kiungo mpya, Larry Bwalya kutokea Klabu ya Lusaka Dynamos ya nchini Zambia ni miongoni mwa usajili bora ambao umefanyika kutokana na uwezo mkubwa anaouonyesha kiungo huyo katika viwanja vya mazoezi vya Simba Mo Arena vilivyoko Bunju jijini Dar.

 

Simba ilianza rasmi mazoezi ya kujiandaa na msimu wa 2020/21, Agosti 17 huku wachezaji wote saba wapya wakiwa sehemu ya mazoezi hayo na kuwapagawisha mashabiki wa timu hiyo ambao wamekuwa wakikusanyika kwa wingi kuwashuhudia.

 

 Fraga amesema: “Naupongeza uongozi kwa usajili bora ambao wameufanya kuelekea msimu ujao, baada ya kupata nafasi ya siku chache kufanya mazoezi na nyota wapya waliosajiliwa kwa upande wangu nadhani usajili huu utazidi kutufanya bora zaidi.

 

“Nimevutiwa sana na uwezo mkubwa wa kiungo wetu mpya, Larry Bwalya ambaye amekuwa kivutio kikubwa kutokana na kipaji cha soka alichonacho, naamini tutakuwa imara zaidi tutakapocheza pamoja,” amesema Fraga.


Bwalya amekuwa kipenzi cha mashabiki kwa muda mfupi kutokana na uwezo wake anaounyesha ndani ya uwanja. Kwenye tamasha la Simba day, Agosti 22 alikuwa ni miongoni mwa nyota waliofanya vizuri mchezo wa kwanza wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya Vital’0 ya Burundi.


Simba ilishinda mabao 6-0 yeye alitoa pasi moja ya bao lililopachikwa kimiani na Bernard Morrison.


Fraga pia alikuwa miongoni mwa viungo waliofanya vizuri. Msimu uliopita alikuwa na ushkaji pia na kiungo mwenzake Deo Kanda raia wa Congo ila msimu huu sio miongoni mwa wachezaji wa kikosi cha Simba kwa kuwa hakuongezewa mkataba.

SOMA NA HII  AZAM FC KAMILI GADO KUWAVAA WAETHIOPIA KIMATAIFA