Home Uncategorized TUIPE SAPOTI TIMU YETU YA TAIFA TUWEKE KANDO TOFAUTI ZETU

TUIPE SAPOTI TIMU YETU YA TAIFA TUWEKE KANDO TOFAUTI ZETU



TAYARI kikosi cha Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars kimeingia kambini Oktoba 5 ikiwa ni maandalizi ya mechi ya kirafiki iliyo kwenye kalenda ya FIFA.

 Etienne Ndayiragije ambaye ni Kocha Mkuu wa timu ya Taifa ya Tanzania ameona wachezaji ambao anawahitaji na kuwaita.Wachezaji 25 wameitwa kwa ajili ya kupeperusha Bendera ya Taifa.

Hapo ninaona kwamba wengine wamegeuka kuwa makocha. Kelele zile za kwamba mchezaji fulani hajaitwa zimeanza kusikika huko mtaani.Hilo jambo ninaona inabidi liachwe tu kwani mwalimu anajua kile ambacho anakihitaji.

Kuwa mwalimu haina maana haufanyi makosa hilo lipo lakini kwa yale aliyoamua acha asimamie kile anachokiamini kwa kuwa ana taaluma katika masuala ya ufundishaji.

Tuna mwalimu ambaye analitambua soka la Tanzania na namna wachezaji walivyo. Labda wapo ambao wamesahau kwamba Ndayiragije alikuwa ndani ya Mbao FC wakati ule ikiwa Ligi Kuu Bara.

 Haikuishia hapo alionyesha uwezo ndani ya Klabu ya KMC ambapo ilimaliza ligi ikiwa nafasi ya nne kwenye msimu wake wa kwanza ndani ya ligi.

Pia alipata nafasi ya kuifundisha timu ya Azam FC. Hapo bado sina mashaka na mwalimu labda aina ya mfumo ambao amekuwa akiutumia mara nyingi kuwa mgumu kupata mabao mengi.

Rekodi zake zinaonyesha kuwa alipokuwa ndani ya Klabu ya KMC alikuwa ni bingwa wa kulazimisha sare hii inatokana na faslasa yake hivyo kwa kuwa ni mwaka mwingine na tutakuwa nyumbani imani yangu ni kwamba atafunguka na atalinda pia.

Uwezo wake ni mzuri sina mashaka nao kwani vikwazo vingi ameweza kuvivuka licha ya ubutu wa safu ya ushambuliaji ambalo ni janga la taifa linahitaji kutafutiwa ufumbuzi hasa kwa wachezaji kuwa makini.

Kwa sasa tunaona kwamba hata kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara inayoendelea wazawa wengi wanaburuzwa na wageni. Hili halipendezi kwani hakuna mshambuliaji halisi mzawa mwenye mabao zaidi ya matatu.

Ukianza kutazama kwa haraka wachezaji wanaoongoza kwa kucheka na nyavu ni wageni hili inabidi liwashtue wazawa nao wajenge urafiki na kucheka na nyavu.

Ninatambua kwamba Ndayiragije anawajua wachezaji wengi ndio maana ana mchanganyiko wa wale wakongwe ambao wana uzoefu kwa muda mrefu kwenye ligi pamoja na mashindano ya kimataifa kiujumla.

SOMA NA HII  AZAM FC MZIGONI LEO KAGAME KUMENYANA NA KCCA

Kwa juhudi zake za kutafuta mafanikio kwenye soka letu ni muhimu kumpa sapoti na kuwa naye bega kwa bega ili kuweza kufikia mafanikio ambayo tunayahitaji wote.

Tumpe sapoti watanzania tusimtenge kwa kumuachia mzigo mzito kwani kufundisha timu peke yako bila sapoti ya mashabiki haileti ile morali ya ushindani jambo ambalo linaumiza kwa mwalimu na wachezaji pia.

Tushikamane kwelikweli katika hili bila kuleta zile itikadi ambazo hazina maana kwa mashabiki na wadau wa soka haitapendeza katika hilo inamaliza uhondo wa mpira.

Tutoe tofauti zetu na kuziweka kando sisi wote ni ndugu na tuna kazi ya kufanya kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu ambalo bado linasaka maendeleo kwa sasa kusonga mbele zaidi ya hapa.

Kila kitu kinawezekana kwa wachezaji wetu kupata matokeo kwani Jumapili sio mbali ambapo wapinzani wetu kutoka Burundi watashuka Uwanja wa Mkapa kukipiga.

Wachezaji ambao mmeitwa ni kazi yenu kupambana kwa hali na mali kuona namna gani timu itapata ushindi kwenye mchezo huo muhimu.

Kikubwa kujituma kwa wachezaji  ndani ya uwanja kutasaidia kupatikana kwa matokeo haraka tukiwa nyumbani kwani uwanja wetu tumeshauzoea na mashabiki zetu tunajua wanataka nini.

Wachezaji majukumu yenu uwanjani haina haja ya kuleta ubishoo ni mwendo wa kazi mwanzo mwisho kutafuta heshima na matokeo ndani ya uwanja kishujaa.

Kwa sasa miguu yenu imeshikilia furaha ya mashabiki na taifa kiujumla mnapaswa mtumie vema maelekezo ambayo mnapewa kutimiza majukumu kwa wakati.

Kile mnachofundishwa kikae akilini na wakati mwingine mambo yakiwa magumu basi kuna umuhimu wa kutumia mbinu ya pili kutafuta matokeo uwanjani ili kuweka heshima.

Hakuna ambaye anafikiria kuona tena wachezaji mtakuwa na papara mkiwa langoni yale makosa yaliyopita mnapaswa myarekebishe kwa kiwango kikubwa.

Mashabiki  wanahitaji kuona timu inapata matokeo na kuwa na morali ya kuendelea kujitokeza kwenye mechi nyingine msiwaangushe mashabiki zetu na taifa kwa ujumla.

Benchi la ufundi kazi kwenu kuwapa mbinu mbadala mkikumbuka kwamba ikiwa wachezaji watapoteza itakuwa ni maumivu kwa mashabiki na taifa kiujumla.

Kila kitu kinawezekana ni wakati wa kuwapa furaha mashabiki ambao watajitokeza uwanjani.Mashabiki pia mjitokeze kwa wingi.