Home Simba SC BOCCO NI MKOMBOZI, TANZANIA INAWAHITAJI WENGI ZAIDI

BOCCO NI MKOMBOZI, TANZANIA INAWAHITAJI WENGI ZAIDI

 


HUENDA ingekuwa si tatizo la majeraha ya mara kwa mara ambayo yanamuandama nahodha wa Simba, John Raphael Bocco, mshambuliaji pekee ambaye amefunga zaidi ya mabao 100 ndani ya Ligi Kuu Bara kwa sasa tungekuwa tunaimba wimbo mwingine.


Bocco amekuwa ni nguzo ndani ya Simba nyakati ngumu wakati timu hiyo ikihitaji matokeo katika Ligi ya Mabingwa Afrika hata ndani ya ligi amekuwa na asili hiyo.


Ukumbuke mchezo uliochezwa Uwanja wa Kambarage wakati ubao ukisoma Mwadui 0-1 Simba, alikuwa Bocco aliyeamua pointi tatu zikaenda kwao.


Ikumbukwe pia wakati Simba ikipambana kuweza kuandika ndoto za kutinga hatua ya nusu fainali mbele ya Kaizer Chiefs ikiwa na mzigo wa mabao 4-0 ni Bocco alianzisha safari katika nyakati ngumu ila haikuwa bahati kwa Simba kwa kuwa aggregate kwa sasa inasoma Simba 3-4 Simba.


Ukiachana na mchezo wa Mei 22, wakati ubao ukisoma Simba 3-0 Kaizer Chiefs na huku mabao hayo yakipachikwa dakika ya 24 na 56 huku lile la tatu likipachikwa na Clatous Chama dakika ya 86, bado Bocco amezidi kuandika rekodi katika mashindano ya kimataifa.


Rekodi zake nyingine za Bocco nyakati ngumu ilikuwa namna hii:-


Nkana 2-1 Simba


Desemba 15,2018, Uwanja wa Nkana ikiwa ni raundi ya kwanza Ligi ya Mabingwa Afrika nyakati zile ngumu, John Bocco alionyesha maana halisi ya kuwa nahodha na mpigania timu.


Wakati Nkana FC ikiwa kwenye ubora wake zama hizo nyota Mtanzania Hassan Kessy ambaye kwa sasa anakipiga ndani ya Mtibwa Sugar yupo huko Zambia. Bocco alianzisha safari ya matumaini kwa Simba kimataifa.


Ni Ronald Kampamba dakika ya 27 na ndugu yake Kelvin Kampamba dakika ya 56 walimtungua kipa namba moja Aishi Manula. Wakati ulimwengu ukiamini kwamba ngoma imeisha, mwanaume Bocco alipachika bao dakika ya 73 kwa mkwaju wa penalti.


Ngoma ilipokuja kupigwa kwa Mkapa, Desemba 23, ubao ulisoma Simba 3-1 Nkana, na watupiaji kwa Simba ilikuwa ni Jonas Mkude dakika ya 29, Meddie Kagere dakika ya 45 na Clatous Chama dakika ya 89 na lile la Nkana lilifungwa na Walter Bwalya na kufanya aggregate kuwa Simba 4-3 Nkana na wawakilishi wa Tanzania wakasonga hatua ya makundi

SOMA NA HII  BAADA YA KUTUA TZ TU...IBENGE KWA MARA NYINGINE KAITAJA SIMBA KWA HILI...AIPA SIFA ZOTE...


Simba 1-0 Al Ahly

Februari 12, 2019 baada ya Simba kutinga hatua ya makundi ilipangwa na mfupa mkavu, Al Ahly ambao walikuwa kwenye ubora wao na wengi waliamini kwamba Simba itapigwa nje ndani.


Uwanja wa Mkapa nahodha Bocco dakika ya 63 alimtengeneza pasi mshikaji wake Meddie Kagere na ubao ukasoma Simba 1-0 Al Ahly. Ilikuwa ni zama za Kocha Mkuu, Patrcik Aussems na Simba ilitinga hatua ya robo fainali kwa kuwa ilimaliza ikiwa nafasi ya pili kwenye kundi.


Simba 2-1 As Vita


Mchezo wa kwanza walipowafuata nchini Congo ubao wa Des Martyrs ulisoma AS Vita 5-0 Simba ilikuwa ni Januari 19, kibao kiligeuka Uwanja wa Mkapa na ilikuwa ni hatua ya makundi suala la msingi pointi tatu ilikuwa ni Machi 16.


Kazadi Kasengu wa AS Vita kwenye mchezo huo wa mwisho kwa Simba Uwanja wa Mkapa alipachika bao la kuongoza dakika ya 13, Mohamed Hussein nahodha msaidizi wa Simba aliweka usawa dakika ya 36.


Wakati AS Vita wakiamini kwamba wameshamaliza shughuli dakika ya 89, Bocco alipiga pasi mpenyezo ikarukwa na nyota wao wa zamani Haruna Niyonzima ambaye kwa sasa yupo Yanga ikakutana na Chama ambaye aliizamisha wavuni mazima.


Itoshe kusema kuwa Bocco ni mshambuliaji asili ambaye kwa namna yoyote ile Tanzania inabidi ijivunie uwepo kwa sasa huku ikiendelea kupiga magoti kuomba akina Bocco wengine zaidi.