Home Makala YANGA MNATAKA TUTENGENEZE ‘HASHTAG’ YA KABWILI?

YANGA MNATAKA TUTENGENEZE ‘HASHTAG’ YA KABWILI?

 


KWA miaka minne sasa kwenye benchi la wachezaji wa akiba wa Yanga kuna jina la golikipa Ramadhani Kabwili, hii ni baada ya kipa huyo kupandishwa kwenye kikosi cha timu ya wakubwa ya klabu hiyo.

Kabwili alipandishwa kikosi cha wakubwa baada ya kuonyesha uwezo mzuri akiwa na timu ya Serengeti boys ilichoshiriki kwa mafanikio michuano ya kombe la mataifa ya Afrika (AFCON), kwa vijana yaliyofanyika nchini Gabon mwaka 2017.

Kabwili anaonekana kuwa kipa wa kawaida sana kwa kuwa tu anasugua benchi pale Yanga, lakini nikukumbushe kuwa huyu ni miongoni mwa walinda mlango wazawa ambao wana vipaji vikubwa vya soka.

Aliweza kulithibitisha hili katika ‘dream team’ ile ya Serengeti boys iliyofanya makubwa katika michuano ya kombe la mataifa ya Afrika kwa vijana mwaka 2017.

Unaweza kujiuliza inawezekanaje kipaji kama cha Kabwili kikaendelea kupotelea benchi? Kama ishu ni uzoefu hiyo haiwezi kuwa hoja yenye nguvu kubwa kwani tayari amefanikiwa kucheza michuano mikubwa ikiwemo michuano ya AFCON ya mwaka 2017.

Lakini amewahi kucheza michezo mikubwa ya Ligi Kuu Bara ikiwemo mchezo wa dabi ya Kariakoo uliopigwa Februari 16, 2019 ambapo Simba walishinda kwa bao 1-0, huku Kabwili akifanikiwa kuonyesha uwezo mkubwa.

Nafasi ya mlinda mlango ndani ya Yanga imekuwa na changamoto kubwa kiasi kwamba mpaka sasa wakiwa wamecheza michezo 31, tayari wameruhusu kufungwa mabao 21, manne kati ya hayo wakifungwa katika michezo miwili iliyopita ambapo kwa nyakati tofauti makipa, Metacha Mnata na Faroukh Shikalo walisimama langoni.

Hali hii imekuwa ikiwakera si tu mashabiki wa Yanga lakini hata wachezaji na viongozi wa klabu hiyo ambao mara kwa mara wameonyesha hasira zao za wazi, na hata kufikia pointi ya kuanza kuangalia uwezekano wa kusajili kipa mpya.

Ni wazi kuwa mpaka sasa Yanga ni miongoni mwa klabu tatu ambazo tayari zimejihakikishia nafasi ya kucheza michuano ya kimataifa kwa msimu ujao, ambapo Tanzania inatarajia kupeleka timu nne katika mashindano hayo ya Ligi ya Mabingwa Afrika na yale ya kombe la Shirikisho.

SOMA NA HII  JINSI WAARABU WANAVYOLIHAMISHA SOKA KWAO....MESSI KAWACHOMOLEA NNJE MAPEMA TU..

Hivyo ni wazi Yanga wanapaswa kufanya jitihada za ziada kumaliza tatizo hili kabla ya kuanza vibarua vya michuano hiyo ya kimataifa, kwa kuwa katika michuano hiyo kuna nyota wengi wa viwango vya juu na kama ni kweli wanataka kushindana na si kushiriki hawana budi kumaliza changamoto kwa kufanya usajili katika maeneo yote ambayo yanaonekana kuwa na mapungufu.

Ni kweli listi ya makipa wa Yanga inahusisha makipa wengi bora, lakini kuelekea michuano hii ya kimataifa unatakiwa kuwa na makipa wa kiwango cha juu zaidi.

Yanga ni lazima waachane na angalau kipa mmoja, na kusajili kipa mwingine mwenye uwezo mkubwa zaidi na uzoefu wa kucheza michuano ya kimataifa.

Lakini pia litakuwa jambo la busara zaidi kumpa nafasi Kabwili ambaye nina uhakika amejifunza mbinu za kutosha, na kilichobaki kwa sasa ni ishu ya kumpa nafasi ya kuthibitisha ubora wake uwanjani, na siyo kusubiri mpaka tutengeneze ‘hashtag’ ya Kabwili.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here