Home news KUMBE! KARIAKOO DABI TATIZO LILIANZIA KWENYE KUITWA WAKUOKOTWA

KUMBE! KARIAKOO DABI TATIZO LILIANZIA KWENYE KUITWA WAKUOKOTWA


WIKIENDI iliyopita, Simba na Yanga zilipambana kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam na matokeo yake ni vijana wa Jangwani waliondoka na ushindi wa bao 1-0.

Kabla ya mechi tambo kibao zilitawala kutoka kwa wasemaji na wawakilishi wa timu hizo. Kila upande ulienda uwanjani ukiwa unaamini unabeba pointi tatu.

Ngoja nikwambie, Simba kama angeshinda mchezo huu sasa hivi angekuwa katangazwa kuwa bingwa wa Ligi Kuu Bara lakini imeshindikana baada ya Yanga kutokubali kuwa zulia lao.


Yanga licha ya kuonekana kama hawapewi nafasi ya kuibuka na ushindi (ilikuwa kuanzia kampuni za kubetisha) hawakutaka kuonekana kama ‘wakuokotwa’ kama walivyokuwa wakiitwa kwa utani na jamaa mmoja hivi.

Utaona hata baada ya mechi, wachezaji wa Yanga walichukua ‘jaba’ na kuanza kuokota makopo ya maji yaliyokuwepo eneo la uwanjani na pembezoni na kisha kuyaweka sehemu ambayo yanatakiwa kuhifadhiwa.


 Utani wa jadi raha sana. Asilimia kubwa ya mashabiki wa Simba waliingia uwanjani wakiamini wanaua, hili ni kosa ambalo hutakiwi kuwa nalo kwenye mechi ya watani. Hii huwa haitabiriki unaweza kuwa bora lakini siku hiyo ikawa tofauti kabisa.


Wakati mechi ikiendelea nilipita mitandaoni kwenye kurasa rasmi za Simba na Yanga kuna moja ya komenti moja ilinivutia ilisema, nanukuu “Yanga wametoa wapi huu mpira, majini haya tunacheza nayo.”

Utaona shabiki kama huyu moja kwa moja alienda na matokeo yake lakini alichokutana nacho ni tofauti ndiyo maana utaona tangu joto la dabi lilivyoanza kupanda Championi tuliandika kuwa usiende na matokeo yako kwani dabi ni kitu kingine unaweza kutana na kitu usichokitarajia.

Yote kwa yote, niwapongeze Yanga chini ya kocha wao, Nasreddine Nabi ambaye ameiongoza timu hiyo kwenye mechi sita ikiwemo ya juzi na kati ya hizo ameshinda nne, sare moja na kupoteza moja hivyo ana rekodi nzuri na kumfunga mtani ni ishu ambayo itazidi kumfanya aimarishe timu yake.


Kocha wa Simba, Didier Gomes yeye tangu atue kikosini hapo jumla ameiongoza timu hiyo kwenye michezo 15, ameshinda 12, sare 2 na kupoteza mmoja ambao ndiyo wa juzi.

SOMA NA HII  YANGA JIANDAENI..PABLO AANZA NA MAMBO MATATU SIMBA..MORRISON NDANI...CHAMPION LEO..

Mechi ilikuwa ya kitofauti na matarajio ya wengi na hii imeendelea kuipa thamani ligi yetu kuwa unaweza kuwa bora zaidi lakini ukashindwa kupata matokeo kwa yule ambaye anaonekana ana ungaunga.

Pongezi kwa Yanga kwa kuonyesha mchezo mzuri na wa tofauti pia kuwafunza wengine kuwa hakuna linaloshindikana na kila kitu kinawezekana.


Kingine kidogo ambacho napaswa kugusia ni ishu ya waamuzi. Katika mchezo huo wa juzi kulikuwa na upungufu kadhaa ambao pamoja na hilo haukuharibu sana maana ya dabi.


Najua wapo wanaosema dabi hutakiwi kutoa penalti lakini mimi ninaona ni sahihi kutoa hata dakika ya kwanza kwa kuwa mchezaji anakuwa ametenda makosa, hivyo tuondoe ile dhana ya kwamba ukitoa kadi mapema basi unaharibu dabi.


Waamuzi wa juzi nadhani wakiangalia marudio ya mchezo wataona makosa ambayo waliyafanya na wanapaswa kuendelea kujisahihisha katika michezo ijayo.


 Unajua linapokuja suala la mwamuzi kuboronga mashabiki na wadau wa soka wamekuwa wakilitupia lawama zaidi Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa namna ambavyo wanawateua waamuzi wa kuchezesha mechi za ligi au mashindano mengine yaliyokuwa chini yao.


 Niseme tu, TFF ni baba la soka Tanzania, lakini imewapa Bodi ya Ligi Tanzania jukumu la kusimamia ligi mbalimbali za hapa na wao ndiyo wanahusika katika kupanga hao waamuzi, hivyo hapa TFF hawapaswi kulaumiwa.