Home news KUNA UWEZEKANO TIMU ZIKABORONGA KIMATAIFA,KAZI NI NGUMU

KUNA UWEZEKANO TIMU ZIKABORONGA KIMATAIFA,KAZI NI NGUMU

 


UWEZEKANO ni mkubwa kwa sasa timu zetu zikaboronga kwenye mashindano ya kimataifa ikiwa hazitajipanga vizuri kutokana na mambo kubadilika kila iitwapo leo.

Tunaona kwamba ni timu tatu ambazo zinatoka Tanzania zimebaki kwenye mashindano ya kimataifa kuondoka kwa mmoja ni pigo ambalo linapaswa kuzibwa na hawa waliopo nao pia wapo kwenye mazingira magumu kwa sasa.

Yanga ambao walikuwa pia katika kuipeperusha bendera ya Tanzania haikuwa bahati kwao licha ya kupambana kusaka matokeo pamoja na mpango wa kuitangaza Tanzania kupitia jezi yao ya mashindano ya kimataifa.

Ukianza kutazama kwenye Ligi ya Mabingwa haya mashindano ambayo ni makubwa kwa hadhi ndani ya bara la Afrika ni Klabu ya Simba imebaki kupambana kwa ajili ya kupata matokeo.

Hapa kazi ni kubwa tofauti na msimu uliopita kwa kuwa kile kikosi cha dhahabu cha Simba kimemeguka na kilichobaki kwa sasa ni kile ambacho kinaundwa kwa mara nyingine.

Haina maana kwamba kikosi cha Simba kwa sasa sio bora hapana ukweli ni kwamba kinapita katika mazingira magumu hasa kutokana na nyota wake wengi kuwa kwenye tatizo la majeruhi.

Ipo wazi kwamba kinachorudisha nyuma maendeleo ya mchezaji ni majeruhi na kinachompasua kichwa kocha kupanga kikosi cha kwanza ni haohao majeruhi.

Hapo inakuwa ni lazima kufanya mabadiliko yasiyo ya lazima ikiwa mchezaji ataanza kwenye kikosi cha kwanza kisha akapata majeraha ama kuamua kusaka mbadala wa mchezaji mwingine ambaye ataweza kuwa kwenye nafasi hiyo ikiwa mchezaji atakuwa anaumwa kabla ya mchezo.

Nimeskiliza maneno ya Kocha Mkuu wa Simba, Didier Gomes kuhusu wachezaji wake kwa kweli katika ulimwengu wa mpira ni lazima aonewe huruma na hapa ambao wanapaswa kumuonea huruma ni wachezaji kwa kutimiza majukumu watakayopewa.

Lakini hapa tunazungumzia katika mashindano ya kimataifa kwa kuwa kama hatua haitachukuliwa kwa wakati huu kuna anguko linakwenda kutokea kwa wawakilishi wetu kimataifa.

Tazama orodha ya wachezaji wake wengi tegemeo kwa sasa bado wanasumbuliwa na majeraha ukianza kwenye safu ya ushambuliaji Chris Mugalu huyu bado hajawa fiti kwa asilimia kubwa.

SOMA NA HII  BAADA YA SIMBA KUMTEMA MKUDE KOCHA WA YANGA KUAMUA JAMBO HILI

Kwa upande wa kiungo Sadio Kanoute na Pape Sakho hawa bado hawajawa imara hii ni ngumu kwa kocha kuwa na furaha kwa namna yoyote ile.

Hata kipa namba tatu Jeremia Kisubi naye anaumwa licha ya mazoezi ambayo anafanya bado hajawa fiti hapa ni lazima wachezaji watimize majukumu yao kwa kujituma wakipewa nafasi kwa kuweza kutambua kwamba Gomes yupo kwenye wakati mgumu na anapenda kuona matokeo yanatokea.

Gomes amesema kuwa alikuwa anatambua umuhimu wa Mugalu lakini hana namna kwa sasa kikubwa ni kuweza kuwatumia hao waliopo kwa umakini na watakaopata nafasi watimize majukumu.

Azam FC nao kwenye Kombe la Shirikisho watambue kwamba wanaanza na mfupa mgumu wa Pyramids hawa nao naona wapo kwenye mvutano na baadhi ya wachezaji licha ya kwamba wachezaji wao ambao wanasumbuliwa na majeruhi ni wachache.

Sawa makosa yapo lakini ni lazima kuyamaliza kwa wakati ili mambo yaweze kwenda kama ilivyo ada wenzentu wa Biashara United hawa wataanza nyumbani basi wapewe sapoti na watimize majukumu yao kwa wakati.