Home Habari za michezo BAADA YA KUSIKIA AZAM WAMEICHAPA NAMUNGO…NABI AWA MWEKUNDU GHAFLA…ADAI MAMBO NI MAGUMU…

BAADA YA KUSIKIA AZAM WAMEICHAPA NAMUNGO…NABI AWA MWEKUNDU GHAFLA…ADAI MAMBO NI MAGUMU…


USHINDI wa mabao 2-1 iliyopata Azam FC dhidi ya Namungo umemshtua Kocha wa Yanga, Nasreddine Nabi aliyesema ni ishara ngumu kwake wakati wakijiandaa kuvaana nao Aprili 6 mwaka huu.

Yanga imemalizana na KMC jana kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa katika raundi ya 18 ya Ligi Kuu Bara kwa kuilaza na mabao 2-0, kisha itarejea tena wiki mbili zijazo uwanjani hapo kumalizana na Azam, ambayo ndio timu ya mwisho kuwatungua wababe hao wa Jangwani kwenye ligi walipowalaza 1-0 kwa shuti la mbali la Prince Dube lililomshinda kipa Faruk Shikhalo aliyepo KMC kwa sasa katika mechi yao ya msimu uliopita iliyopigwa Aprili 25 mwaka jana.

Nabi analiwaza pambano hilo lijalo huku akivurugwa na pointi tatu ilizovuna Azam dhidi ya Namungo na kukiri anapaswa sasa kujipanga zaidi kwani anakutana na timu iliyojengeka morali kutokana na ushindi huo wa ugenini.

“Walianza kufungwa dakika za mapema kabisa lakini baada ya dakika 90 wamesawazisha na kufunga bao la ushindi, timu ya namna hiyo sio ya kuibeza tunahitaji kujipanga ili kuweza kuikabili kwa kuibuka na ushindi kwenye mchezo huo,” alisema Nabi na kuongeza;

“Tuna mechi ngumu ambazo ndio zitaamua matokeo mazuri hadi mwisho wa msimu Azam ni kati ya timu hizo, inapopata matokeo inanishtua na kunihimiza kuliandaa jeshi langu lijipange kwa ushindani.”

Nabi alisema ana nafasi nzuri ya kusuka jeshi lake kabla ya kukutana nao, huku akitaja kuwa ni muda ambao wachezaji wengi waliokuwa majeruhi watakuwa wamesharudi hivyo hatakuwa na visingizio.

“Azam ni timu nzuri ina wachezaji wengi wazoefu nimekuwa nikiifuatilia, mchezo wa juzi na Namungo sikuutazama nilikuwa nawaandaa vijana wangu kwaajili ya mchezo wa leo nitapata nafasi ya kuangalia marudio kujua ubora wao na udhaifu wao kabla hatujakutana,” alisema na kuongeza;

“Kuna mabadiliko makubwa, mzunguko wa kwanza tulipokutana na sasa lazima watakuwa wameongeza kitu hivyo nitakaa na benchi la ufundi kuwasoma upya kwa kuangalia michezo yao miwili au mitatu ili kufahamu namna ya kuwakabili.”

SOMA NA HII  CAF YAWAPA JEURI SIMBA SC...MAZEMBE KWISHAA MASTAA YANGA WAJIPANGA HIVI

Ligi Kuu itasimama ili kupisha maandalizi ya timu ya taifa, Taifa Stars itakayocheza mechi mbili za kirafiki za kimataifa kwa mujibu wa kalenda ya FIFA dhidi ya Sudan na Jamhuri ya Afrika ya Kati zitakazochezwa kati ya Machi 23 na 29 jijini Dar es Salaam.