Yanga wameangalia rekodi zao dhidi ya Coastal Union nje ya Jiji la Tanga wakacheka sana. Timu hizo kwa uchache tangu mwaka 2011 zimekutana mara tisa nje ya Tanga na ushindi mkubwa wa Coastal ni sare mbili lakini zilizosalia zote Yanga ilishinda.
Coastal ambayo ikiwa nyumbani imeambulia ushindi mara tatu, wanashikilia hatma ya mataji yote mawili ya Yanga lile la ASFC na Ubingwa wa Ligi. Timu hiyo ya Kocha Juma Mgunda Juni 15 itaivaa Yanga kwenye Uwanja wa Mkapa katika mechi ya Ligi, siku 16 baadae watakutana tena Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Arusha kwenye mchezo wa fainali wa ASFC utakaochezwa Julai 2.
Coastal Union inayomtegemea, Abdul Suleiman ‘Sopu’ mwenye mabao saba kwenye Ligi Kuu iliisambaratisha Azam mchezo wa nusu fainali kwa kuichapa kwa mikwaju ya penalti 6-5 wakati Yanga ikiiondoa Simba kwa bao 1-0.
Hata hivyo, rekodi tamu ya Mgunda tangu aipokee timu hiyo Aprili 7 mwaka huu imeonekana kuwa tishio kwani katika michezo saba aliyosimamia ameshinda minne na kufungwa mitatu.
Mgunda alisema watapambana kiume, ingawa Nabi Mohammed wa Yanga amejibu kwamba hawaachi kitu na akili yao ya sasa kumalizia mechi mbili zilizobaki kwa ushindi bila kujali wanakutana na nani.
“Nawaheshimu Yanga kutinga kwao kunadhihirisha kwamba ni bora na sisi pia ni bora ndio maana tumetinga hatua ya fainali tunatarajia mchezo mzuri dakika 90 zitaamua nani atatwaa taji,” alisema.
Kocha Nabi alisema anawaheshimu wapinzani wake Coastal ambao amekiri kuwa wamekuwa bora hivyo atakuwa na dakika 180 ngumu lakini lengo la kwanza ni kuendeleza kasi yao na amewakumbusha wachezaji umuhimu wa mechi hizo kwao binafsi na mashabiki wao.
Alisema ameshuhudia mchezo mzuri kwenye nusu fainali kati yake na Azam FC anatarajia kukutana na mechi bora na ngumu kutoka kwao kutokana na wachezaji wa Coastal kuingia kwenye mchezo huo wakiwa na ari baada ya kupata maotokeo.
“Sina hofu kikubwa ninachokiangalia ni kuhakikisha wachezaji wangu wanafanya kile kitakachotupa matokeo mazuri kwenye michezo yote miwili lengo ni kutovunja rekodi ya kufungwa dakika za mwisho,”
“Kwasasa nazingatia kila mchezo ulio mbele yangu sasa nasaka pointi tatu tu nitwae ubingwa wa ligi mchezo wangu unaofuata ni dhidi ya mpinzani wangu kwenye fainali ya ASFC kuhusu pointi za ubingwa hata nisipopata kutoka kwake nafahamu bado nina nafasi ya kupata,” alisema na kuongeza;
“Kwenye mchezo wa fainali ni kuhakikisha napata matokeo ili nitwae taji hivyo dakika 180 natarajia zitakuwa bora na ngumu kwa kila timu kuhitaji matokeo,” alisema Nabi.
TANO ZA MGUNDA TPL
Mbeya Kwanza 2-0 Coastal Union
Polisi 0-1 Coastal Union
Coastal Union 1-0 Biashara
Coastal Union 2-1 Dodoma
Mbeya City 0-1 Coastal Union
TANO ZA YANGA ASFC
RAUNDI YA 2
Young Africans 4-0 Ihefu SC
RAUNDI YA 3
Young Africans 1-0 Mbao FC
RAUNDI YA 4
Young Africans 2-1 Biashara United FC
ROBO FAINALI
Young Africans 1-1 Geita Gold FC (P:7-6)
NUSU FAINALI
Young Africans 1-0 Simba SC
Fei Toto
CCM Kirumba Stadium, Mwanza.
TANO ZA COASTAL ASFC
RAUNDI YA 2
Coastal Union 2-0 Fontein Gate
RAUNDI YA 3
Coastal Union 8-1 TOP Boys FC
RAUNDI YA 4
Coastal Union 2-0 Mtibwa Sugar
ROBO FAINALI
Coastal Union 1-1 Kagera Sugar (P:5-4)
NUSU FAINALI
Coastal Union 0-0 Azam FC (P:6-5)