Home Habari za michezo UKWELI MCHUNGU….KILICHOIGHARIMU SIMBA MSIMU HUU NI PAMOJA NA HAYA….CHAMA, BOCCO NA UONGOZI...

UKWELI MCHUNGU….KILICHOIGHARIMU SIMBA MSIMU HUU NI PAMOJA NA HAYA….CHAMA, BOCCO NA UONGOZI WAHUSIKA…


Msimu umemalizika huku Simba ikiambulia patupu baada ya kushindwa kutetea mataji matatu iliyotwaa msimu uliopita, Ligi Kuu Bara, Ngao ya hisani yaliyochukuliwa na Yanga pamoja na kombe la Shirikisho ASFC.

Simba msimu uliopita ilibeba mataji yote hayo kwa kishindo ila msimu huu yote yamekwenda wa watani wao Yanga ambao jana Jumamosi, walicheza fainali ya Kombe la ASFC dhidi ya Coastal Union kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Arusha na kufanikiwa kubeba taji hilo kwa changamoto ya mikwaju ya penati.

Kuna maeneo ambayo yalikuwa changamoto kwa Simba msimu huu hadi kushindwa kufanya vizuri katika mashindano hayo matatu na kushindwa kuchukua taji lolote huku ikionekana kushindwa kucheza vizuri.

Makala hii inakuletea mambo yaliyochangia Simba kushindwa kufanya vyema kwenye mashindano hayo msimu huu huku watani wao Yanga wakionekana kuwa na kikosi bora katika maeneo mengi.

‘PRE-SEASON’

Msimu huu ulianza kwa kikosi cha Simba kushindwa kuwa na maandalizi mazuri kwani kikosi hicho kilikwenda Morocco ila hakikupata muda wa kutosha kufanya mazoezi ya pamoja kwa sababu mbalimbali.

Wakati Simba inakwenda Morocco ilikutana na janga la uviko 19, likiwa limechachamaa zaidi kwahiyo baadhi ya wachezaji wao walishindwa kufanya mazoezi kwa pamoja kwenye kambi hiyo.

Kuna baadhi ya wachezaji wa Simba waliiitwa katika kikosi cha timu ya taifa, waliondoka hapa nchini kwa makundi jambo ambalo lilichangia kutokuwa na muda mzuri wa kufanya maandalizi japo jambo hili pia liliwakuta mabingwa Yanga ambapo pia walienda Morocco.

USAJILI

Simba ilifanya usajili wa wachezaji zaidi ya kumi kwenye dirisha kubwa la usajili ila kati ya hao wengi wameshindwa kufanya vizuri na kutoa mchango wa kutosha ndani ya kikosi hicho.

Miongoni mwa wachezaji walioshindwa kufanya vizuri, Duncun Nyoni aliyesajiliwa kwa mkataba wa miaka mitatu ila aliishi ndani ya Simba kwa muda wa miezi sita tu na kutolewa kwa mkopo.

Miongoni mwa nyota wachache waliyofanya vizuri waliosajiliwa wakati huo wapo, Henock Inonga, Kibu Denis na Sadio Kanoute huku wengi wao wakionekana kucheza katika viwango vya kawaida.

KUWAUZA CHAMA, LUIS

Kabla ya msimu huu kuanza uongozi wa Simba ulifanya biashara ya kuuza nyota wao wawili wa kikosi cha kwanza, Luis Miquissone aliyekwenda Al Ahly ya Misri na Clatous Chama aliyetua RS Berkane ya Morocco.

Hadi msimu unamalizika pengo la Luis halikuonekana kupata mchezaji sahihi wa kuliziba licha ya kikosi hicho kusajili mawinga wengi kama, Yusuph Mhilu, Pape Sakho na Pater Banda.

Kushindwa kuzibwa kwa pengo hilo la Luis, viongozi wa Simba walilazimika kutumia pesa nyingi kumrudisha Chama katika kikosi hicho kwenye dirisha dogo la usajili ingawa naye alishindwa kufanya vizuri kutokana na majeraha ya muda mrefu.

UBORA WA KIKOSI

SOMA NA HII  SIMBA WAAPA...WATAJUA HAWAJUI...BARBARA AANIKA MBINU NZITO..MWANASPOTI....

Msimu uliopita kikosi cha Simba kilikuwa na wachezaji wengi ambao kila mmoja kwa nafasi yake alikuwa na ubora kutokana na eneo ambalo alikuwa analitumikia kwa kutimiza majukumu yake ya kazi vizuri.

Mfungaji bora msimu uliopita alitokea Simba, John Bocco akiwa na mabao 16, huku Chriss Mugalu akiwa na 15 wakati Meddie Kagere alimaliza na 14 bila kusahau Chama na Luis peke yao wawili walihusika moja kwa moja katika mabao 43 (Chama alifunga 8 asisti 15, Luis alifunga tisa asisti 11). Kuyaondoa mabao 40+ kikosini ilikuwa ni pigo kubwa Simba.

Msimu uliopita, kikosi cha Simba kilitoa mchezaji bora wa msimu (Bocco), kipa bora wa msimu (Aishi Manula) na kilikuwa na wachezaji wengi waliounda kikosi bora cha msimu kutokana na viwango bora walivyoonyesha, lakini jambo hilo halitarajiwi msimu huu.

Ukiachana na wachezaji hao kuna wengine walikuwa na mchango wa kutosha na kusababisha timu hiyo kufanya vizuri kama, Hassan Dilunga, Mohammed Hussein, Shomary Kapombe, Pascal Wawa, Joash Onyango, Jonas Mkude na wengineo wengi.

Msimu huu mambo yamekuwa tofauti mfungaji bora wa Simba kabla ya mzunguko wa mwisho kuchezwa alikuwa ana mabao 8 Kibu akifunga nusu ya yale aliyofunga Bocco msimu uliopita.

Simba ilijikwaa hapo hawakuwa na wachezaji wengi waliokuwa bora katika kutimiza majukumu ya nafasi zao tofauti na msimu uliopita.

BENCHI LA UFUNDI

Msimu huu Simba imefanya mabadiliko ya makocha watatu kwa nyakati tofauti, jambo ambalo si zuri kwa timu yenye kuhitaji mafanikio ndani ya msimu kufanya mabadiliko makubwa kama hayo.

Simba ilianza msimu ikiwa na kocha, Didier Gomes na baada ya kuondolewa kwenye hatua ya mtoano Ligi ya Mabingwa Afrika iliachana naye na kikosi kilikuwa chini ya kocha mkuu wa muda, Hitimana Thierry.

Baada ya muda ligi ikiwa katikati Simba ilimchukua Pablo Franco kukiongoza kikosi hicho ila waliachana na Hitimana ambaye alionekana kutokuwa na maelewano mazuti kati yake na kocha mkuu.

Simba baada ya kushindwa kufanya vizuri kabla ya msimu kuanza iliachana na Pablo kisha timu hiyo kubaki na kocha wa muda, Selemani Matola aliyemaliza msimu na kikosi huku kuna baadhi ya mechi alifanya vizuri nyingine alishindwa.

UONGOZI

Msimu huu moja ya maeneo ambayo Simba ilikuwa na changamoto nayo ni kushindwa kuwa na utulivu katika uongozi kwani kuna muda vitu fulani viliendelea chini kwa chini hadi kushindwa kufanya vizuri.

Kuna baadhi ya viongozi wale wa mstari wa mbele kuipigania timu waliondoka katika harakati hizo na kubaki wachache, ilikuwa ngumu kwa kufanya vizuri tofauti na ilivyokuwa kwa wapinzani wao Yanga.

Halikuwa jambo la kushangaza msimu huu wachezaji wa Simba wanaenda kucheza na Yanga hakuna ahadi yoyote ya bonasi.