Home Habari za michezo HARAKATI ZA USAJILI ZAANZA RASMI YANGA…NABI AKABIDHI MAJINA YA VYUMA 5 KWA...

HARAKATI ZA USAJILI ZAANZA RASMI YANGA…NABI AKABIDHI MAJINA YA VYUMA 5 KWA HERSI…

Kikosi cha Yanga SC

Mabosi wa Yanga wamekabidhiwa majina matano ya wachezaji ambao Kocha Mkuu wa timu hiyo, Mtunisia Nasreddine Nabi amependekeza kwa ajili ya kuwaongezea mikataba mingine mipya ya kuendelea kubakia kikosini hapo.

Hiyo ni katika kuelekea usajili wa dirisha dogo litakalofunguliwa mapema Desemba, mwaka huu ambao Yanga wamepanga kukifanyia maboresho kikosi chao kwa ajili ya hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Yanga imepanga kukifanyia maboresho makubwa kwa kufanya usajili mkubwa wa kisasa kwa kuanza na nyota wao ambao mikataba yao inaelekea ukingoni.

Baadhi ya wachezaji wanaotajwa kupendekezwa kuongezewa mikataba mipya mingine ni Zawadi Mauya, Denis Nkane, Djigui Diarra, Jesus Moloko na Abdultwalib Msherry.

Rais wa timu hiyo, Injinia Hersi Said alisema kuwa tayari wamepokea majina ya wachezaji ambao kocha amependekeza kuongezewa mikataba mipya baada ya kuvutiwa na viwango vyao.

Hersi alisema kuwa wapo katika hatua za mwisho na wachezaji hao waliopendekezwa na kocha huyo kwa ajili ya kuwaongezea mikataba hiyo, kila kitu kinakwenda vizuri na walichobakisha ni kusaini mkataba pekee.

Aliongeza kuwa hawatakuwa na orodha kubwa ya wachezaji wapya watakaowasajili katika dirisha dogo zaidi watawaboreshea mikataba hao nyota wao wa zamani kocha aliowahitaji.

“Tumejipanga vema kufanya usajili mzuri dirisha dogo hili kujazia tu baadhi ya nafasi ambazo kocha Nabi ametuambia.

“Lakini kabla ya kuanza usajili mpya dirisha dogo kuna baadhi ya wachezaji ambao tutakwenda kumalizana nao kwa kuwaongeza mikataba mipya ya kuendelea kubakia hapa Yanga.

“Na hivi karibuni tutawapa mikataba hiyo mipya, tupo katika mazungumzo nao kwa sasa na kila kitu kinakwenda sawa,”alisema Hersi.

SOMA NA HII  BAADA YA KUKIWASHA VILIVYO MTIBWA....NDEMLA KURUDI MJINI KIULAINII...DOMAYO, MBOMBO KUMPISHA AZAM....