Home Habari za michezo ACHANA NA MECHI YA YANGA vs USMA….KIPUTE CHA UKWELI NI HIKI HAPA...

ACHANA NA MECHI YA YANGA vs USMA….KIPUTE CHA UKWELI NI HIKI HAPA ‘MZEE BABA’…WABABE WATUPU YANI..

Al Ahly vs Wydad

KWA mara ya tatu katika historia, Al Ahly ya Misri na Wydad Athletic Club ya Morocco zitamenyana katika fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika (CCL) ambayo inatarajiwa kuchezwa Juni 4 na 11, Cairo na Casablanca.

Huu ni msimu wa 59 wa michuano hiyo ya kimataifa ambayo huandaliwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF) na ni awamu ya 27 tangu kuanza kutambulika kama Ligi ya Mabingwa Afrika. Tofauti na misimu mitatu iliyopita, fainali ya msimu huu itachezwa nyumbani na ugenini kulingana na uamuzi wa CAF kwenye kikao cha kamati ya utendaji Julai 3 huko Rabat.

Yote hiyo ni kutokana na malalamiko rasmi yaliyotolewa na Al Ahly kwa CAF kuhusu uchaguzi wa Stade Mohammed V mjini Casablanca kama uwanja wa fainali ya 2022: licha ya nia ya kwamba fainali ichezwe katika uwanja usio na upande wowote, mashindano ya 2022 yalifikia kilele kwa uwanja kuwa uwanja wa nyumbani wa mpinzani wao, Wydad AC.

Turudi kwenye mstari, wakiwa nyuma ya Mamelodi Sundowns mara mbili, Wydad walining’inia na kufanikiwa kusawazisha na mchezo huo kumalizika kwa sare ya mabao 2-2 hivyo kuwa na faida ya bao moja la ugenini na kutinga fainali nyingine ya Ligi ya Mabingwa Afrika. Wamorocco, ni mabingwa watetezi, watakutana na mpinzani sawa na msimu uliopita, Al Ahly.

Hii itakuwa mara ya tatu kwa timu hizo mbili kumenyana katika hatua hii ya kinyang’anyiro baada ya 2017 na 2022. Ingawa inaweza kushangaza, ni Wamorocco walioshinda fainali mbili zilizopita dhidi ya wababe hao wa Al Ahly.

Kwa upande wa Misri, waliotwaa taji mara 10 katika shindano hilo, itakuwa fainali ya sita awamu saba ziliyopita.
Wamepigwa mwaka jana na WAC (2-0), Wamisri tayari wamepoteza fainali mbili mfululizo 2017 na 2018.

Je, Al Ahly watamaliza gundu walilonalo dhidi ya Wydad? WAC, kwa vyovyote vile, haijawahi kushinda taji hilo mara mbili mfululizo (1992, 2017, 2022). Makala hii inakuletea wachezaji ambao wanaweza kuuamua mchezo huo.

MAHMOUD SOLIMAN
Huu ni mtambo wa mabao wa Al Ahly, anafukuzia kiatu cha ufungaji bora, anashika nafasi ya pili kwenye orodha hiyo akiwa na mabao matano sawa na Hamza Khabba wa Raja Casablanca nyuma ya kinara Peter Shalulile mwenye mabao sita wa Mamelodi Sundowns ambayo iliishia hatua ya nusu fainali.

Solimani amewahi kucheza soka la kulipwa Ulaya akiwa na Luzern, Grasshopper za Uswisi, Desportivo das Aves ya Ureno na Hatayspor ya Uturuki hivyo ni mshambuliaji mwenye uzoefu wa kutosha.

BOULY SAMBOU
Ndiye kinara wa mabao wa Wydad Casablanca idadi yake ya mabao manne ni sawa na Clatous Chama na Jean Baleke wa Simba, raia huyo wa Senegal amekuwa akitegemewa na miamba hiyo ya Morocco kwenye safu yao ya ushambuliaji.

Sambou mwenye miaka 24 anaweza kusimama kama mshambuliaji wa mwisho, muda mwingine anaweza kutokea pembeni kama winga upande wa kushoto au kulia hivyo atatoa wigo mpana kwa Sven Vandenbroeck jinsi ya kumtumia kwenye fainali.

PERCY TAU
Hakuna shaka hata kidogo kuwa nyota wa Bafana Bafana, Percy Tau ni mmoja kati ya wachezaji bora Afrika Kusini. Hata hivyo, kwa miaka kadhaa iliyopita, fowadi huyo wa Al Ahly amevumilia nyakati ngumu.

Hata hivyo, mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 29 anaonekana kurejea kwenye ubora wake. Winga huyo ndiye aliyeibeba Al Ahly kwenye mchezo wa nusu fainali ya kwanza kwa kufunga mabao mawili dhidi ya ES Tunis kwenye ushindi wa mabao 3-0 wakiwa ugenini, ni kama alihitaji nafasi zaidi ya kucheza ili kurejea kwenye kiwango chake kwani hakuwa akipata nafasi ya kutosha pale Brighton.

Katika moja ya mahojiano yake aliwahi kueleza,”Kuna umuhimu gani wa mimi kukaa (Brighton) wakati sichezi? Kila mtu anataka kuniona nikicheza , nataka kujiona nikicheza na familia yangu inataka kuniona nikicheza.”

ARSENE ZOLA
Ni mzaliwa na Lubumbashi pale DR Congo, anatajwa kuwa mmoja wa mabeki bora kwenye ligi ya Morocco maarufu kama Batola Pro, ni mtulivu akiwa na mpira mguu hata wakati akitekeleza majukumu yake ‘kuzuia’ pia hata kazi chafu anaziweza.

Takwimu zake zinaonyesha amecheza michezo 36 msimu huu, ikiwemo 12 ya Ligi ya Mabingwa Afrika na kufunga mabao matatu, kuonyesha kuwa nidhamu yake ni kubwa kwenye michezo yote hiyo ameonyeshwa kadi moja tu ya njano, hana kadi nyekundu.

HUSSEIN EL SHAHAT
Licha ya kuwa ni winga amefunga mabao manne kwenye mashindano hayo msimu huu sawa na Tau, pia anaweza kucheza kama namba 10.

El Shahat ambaye amekuwa akiitumikia Al Ahly tangu 2019, ni kati ya wachezaji hatari wa miamba hiyo ya soka la Afrika hivyo Sven na vijana wake wanatakiwa kuwa naye makini vinginevyo anaweza kuwatibulia mipango yao.

YAHYA JABRANE
Ni mshindi mara tatu wa Ligi Kuu Morocco ‘Batola Pro’ na mchezaji bora ligi hiyo mara moja, alitwaa mara mbili Kombe la CHAN akiwa na timu yake ya taifa la Morocco pia ametwaa mara moja Ligi ya Mabingwa Afrika.

Ndiye nahodha wa Wydad Casablanca, amekuwa akifanya vizuri eneo la kiungo licha ya kuwa na uwezo pia wa kucheza kama beki wa kati, ni mchezaji kiungo na uzoefu wake unaweza kuwa faida kwa vigogo hao.

SOMA NA HII  KADUGUDA:- VIONGOZI WA SIMBA HII WAMEFELI MAENEO MENGI ...UKISEMA INAKUWA NONGWA...