Home Habari za michezo BADALA YA KUANZA KULALAMIKA…SIMBA WAANZE NA ALIYEMTOA KAKOLANYA GOLINI…

BADALA YA KUANZA KULALAMIKA…SIMBA WAANZE NA ALIYEMTOA KAKOLANYA GOLINI…

Golikipa wa Simba SC chaguo la Pili David Kakolanya kujiunga na Azam FC

Ukifuatilia wadau na mashabiki wa Simba wamekuwa kila mmoja na kilio chake juu ya hatua ya timu hiyo kuondolewa katika mashindano mbalimbali huku pia ikiwa na uwwezekano mdogo wa kuchukua ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu.

Hatua hiyo inakuja kufuatia Simba kupoteza nafasi ya kuchukua taji la Ligo ya Mabingwa wakitupwa nje na bingwa mtetezi Wydad Athletic ya Morocco katika mechi ambayo wengi walidhani Simba ingewashangaza wengi kwa kuwang’oa Waarabu hao.

Kama haotoshi wikiendi iliyopita ikatolewa kwenye Nusu Fainali ya ASFC wakifungwa kwa mabao 2-1 dhidi ya Azam FC na sasa kubakiza mechi zao za ligi pekee kumaliza msimu wakiendelea kuifukuza Yanga ambao ndio vinara wanaonekana kupewa nafasi kubwa ya kuchukua ubingwa.

KIKOSI CHA KAWAIDA Safari ya Simba kutupwa nje yanasemwa mengi lakini kubwa litabaki kuwa aina ya kikosi walichonacho msimu huu hakikuwa na ubora wa kuweza kuipigania Simba ndani ya uwanja kiubora kulingana na hadhi ya klabu hiyo.

Ukweli usipingika kuwa Simba inatakiwa kuanza kujipanga sasa kuachana na wachezaji wengi ambao wanaonekana kutupwa na umri, wengine wakiwa na uwezo wa kawaida licha ya umri wao kuwa wa kawaida kuweza kushindana lakini daraja walilonalo haliendani na kasi ya ushindani kuipigigania jezi ya klabu hiyo.

ISHU YA SALIM GOLINI KAKOLANYA NJE

Ukiacha hoja hizo kubwa lakini ishu nyingine kubwa ambayo imewalazimisha Simba kuanguka ziadi ni matumizi ya kipa wao namba tatu Ally Salim ambaye alianza kutumika tu baada ya kuumia kwa kipa wao chaguo la kwanza Aishi Manula.

Kwanza nimpongeze Salim kwa moyo wake wa uthubutu aliouonyesha katika mechi ambazo alicheza, alionyesha kuwa na roho ngumu akianza kuaminiwa katika mechi ngumu dhidi ya Yanga wekundu hao wakishinda lakini pia mchezo wa Wydad wa hapa kisha baadaye kuonyesha dosari chache zikaanza kuonekana.

Mengi yataongelewa lakini uamuzi wa kumtumia Salim ambaye hajaonekana langoni kwa Simba kwa misimu zaidi ya miwili akishindwa kucheza hata mechi mbili ulikuwa uamuzi mgumu na wa kikatili kwa Simba.

Tukumbuke wakati uamuzi wa kumtumia Salim ulikuja kwa kile kilichoelezwa kuwa kipa wa Simba namba mbili Beno Kakolanya amesaini klabu nyingine na kwamba baadhi ya vigogo wa klabu hiyo wakidhani anaweza kuwafungisha kirahisi katika mechi za timu hiyo.

WAKAMUWEKA BENCHI

Swali ambalo limewashangaza wengi kwa uamuzi huo ni kuwa licha ya vigogo hao kuona mashaka ya kumtumia Kakolanya lakini bado wakamuweka kambini, wakafanya naye mazoezi lakini kubwa akawa kipa chaguo la pili benchi endapo Salim ataumia.

Hapa unaanza kupata mashaka na aliyefanya uamuzi huu kwamba kama Kakolanya anafaa kuwa benchi anashindwaje kuaminika kucheza kwa kuwa suala la kuingia lilikuwa wazi pale tu Salim akipata maumivu au akitolewa kwa hatua zingine za kimchezo.

MAKOSA YA SALIM

Hakuna maana kwamba Kakolanya hafungiki lakini anafungwa tu kama kipa mwingine lakini kwa mabao ambayo Salim aliyaruhusu kuanzia bao la Wydad ugenini kisha mabao mawili dhidi ya Azam ambayo yote yaliwatoa Simba kwenye mashindano sio rahisi sana kuona makosa kama yale kwa Kakolanya.

Kakolanya ni kipa aliyekomaa na ameshacheza mechi nyingi za Kimataifa na hata ndani angewasaidia zaidi Simba kutoka salama kuliko maamuzi ambayo yalifanyika hii ilikuwa shida kubwa ambayo iliwafanya Simba kupotea zaidi.

MABEKI WALIHITAJI KUMLINDA SALIM

Salim kuwa salama langoni haikuwa rahisi ilihitaji mabeki kufanya kazi kubwa ya kumlinda zaidi ili asikutane na nyakati ngumu ambazo zingeiharibia hesabu Simba, hili kiufundi liliwapunguzia kasi ya timu kusogeza mashambulizi mbele zaidi.

SIMBA IKASAJILI KIPA BORA ZAIDI

Endapo Kakolanya hataweza kubaki Simba basi kuna haja kubwa kwa Simba kwenda kutafuta kipa mwingine mwenye ubora zaidi ya Manula na Salim katika kuimarisha eneo lao hili muhimu.

Ukiangalia utaona kwa ndani sio rahisi kupata kipa anayemzidi Manula kwa kuwa mshindani bora alikuwa ni Kakolanya ambaye hata alipokuwa anaingia golini kulikuwa hakuna wasiwasi mkubwa kama ambavyo ilijitokeza kwa Salim.

Hesabu zinailazimisha Simba kutoka nje ya nchi kutafuta kipa mwingine bora ambaye atakuja kushindania nafasi na Manula hii itazidi kumuongezea ubora Manula lakini pia itaifanya idara hiyo kuwa imara zaidi kisha wawili hao chini yao awepo Salim.

Salim hatakiwi kupoteza kipo kitu kikubwa amekionyesha na kinatakiwa kuthaminika kwa kuwa ameonyesha ujasiri wote huo akiwa anatokea kwenye chaguo la tatu, kitu kikubwa kinachotakiwa kufanyike kwake zipo mechi anatakiwa kuendelea kupewa au hata muda wa kucheza kidogokidogo akiendelea kujengwa na kuja kuwa imara zaidi.

Nyakati hazisimami kuna wakati kina Manula wataondoka, watakaokuja kuchukua nafasi ni hawa kina Salim hatutakiwi kuwapoteza tunatakiwa kuendelea kuwajenga kupitia mapungufu yakiyojitokeza ili waje kuwa Kina Manula bora kwa Simba na Taifa siku za mbele.

SOMA NA HII  KISA USHINDI KIDUCHU DHIDI YA VIPERS...'TSHABALALA' AWAPA ZA USO MASHABIKI WANAOPONDA...