Home Habari za michezo HATIMA YA MAYELE NA YANGA IKO HIVI…ATAKA MSHAHARA WA MILI 53 KWA...

HATIMA YA MAYELE NA YANGA IKO HIVI…ATAKA MSHAHARA WA MILI 53 KWA MWEZI…ADA YA USAJILI BIL 1…

Tetesi za Usajili Yanga

Siri imefichuka! hivyo ndiyo unavyosema kusema baada ya taarifa kutoka Afrika Kusini kueleza kiwango cha mshahara ambacho mshambuliaji wa Yanga, Fiston Mayele anataka apewe ili atue Kaizer Chiefs.

Mayele amekuwa kwenye ubora wa hali ya juu msimu huu akiwa amemaliza kinara wa mabao Ligi Kuu Bara baada ya kufunga mara 16, huku akiwa pia kinara kwenye Kombe la Shirikisho Afrika ambalo timu yake ipo fainali akifunga mabao saba.

Taarifa mbalimbali zimekuwa zikisema kutakuwa na ugumu wa Yanga kumzuia Mayele kuondoka baada ya msimu huu kumalizika, huku gazeti kubwa la Far Post la Afrika Kusini likieleza mchezaji huyu mshahara wake anataka ni milioni 53.

Gazeti hilo ambalo linafuatiliwa na wasomaji wengi Afrika Kusini, jana liliandika habari hiyo, huku likieleza ni kwa nini Kaizer Chiefs itakuwa rahisi kwao kumpata mshambuliaji wa Marumo Gallants, Ranga Chivaviro kuliko Manyele.

Kaizer Chiefs, wana mpango wa kuboresha kikosi chao kwa ajili ya msimu ujao na Mayele ni mmoja kati ya wachezaji inayowataka kwa kuwa staa wao Caleb Bimenyimana anatarajiwa kuondoka baada ya kushindwana na Kocha Arthur Zwane.

Baada ya timu hiyo kugundua mchezaji huyo anaondoka, gazeti hilo limesema Kizer ambayo ni timu maarufu kwenye ligi hiyo imeweka majina mawili mezani kwao Mayele na Chivaviro wa Marumo Gallants, lakini wao wanampa nafasi kubwa Chiva kutokana na mshahara wa Mayele kuwa mkubwa.

Wamesema endapo Kaizer watamchukua Mayele mwenye miaka 28, watatakiwa kutoa kitita cha randi 450,000, sawa na Sh53 milioni, huku wakisema mchezaji huyo kwa sasa akiwa na Yanga analipwa milioni 21 kila mwezi.

Hata hivyo, wamesema gharama ambayo Kaizer wameelezwa ya usajili wa ni randi 10 milioni, sawa na Sh1 bilioni, kiwango ambacho wanaona kitakuwa kikubwa kwao kukitoa kwa staa huyo.

“Mshahara wake ni R450,000, kwa mwezi kwa kuwa ni mchezaji mwenye soko kubwa zaidi kwa sasa kutokana na uwezo ambao ameouonyesha kwenye michuano ya Afrika msimu huu, hii inaonekana ni fedha nyingi kwa mchezaji ambaye anakuja kuwa mpya kwenye DStv Premiership. Tumeona huko nyuma wachezaji waliofanya vizuri kwenye ligi nyingine, hawana uhakika wa kufanya vizuri hapa PSL,” liliandika gazeti hilo.

Gazeti hilo limemtolea mfano Bimenyimana pamoja na mshambuliaji raia wa Congo, Christian Saile, ambao walikwenda kwenye ligi hiyo na kushindwa kufanya vizuri pamoja na kwamba walipotoka walikuwa wakali.

Far Post, limeendelea kusema mshahara wa Chiva na Mayele utakuwa tofauti, lakini wanaamini pia mshambuliaji huyo raia wa Afrika Kusini anaweza kuwa na msaada mkubwa kuliko Mayele kwa kuwa tayari ana uzoefu kwenye ligi hiyo ya PSL.

“Chiva atakwenda Kaizer bure, tayari timu yao imeshashuka daraja na huyu ni mmoja kati ya wachezaji ambao itaamua kuwaachia waondoke kwa kuwa alisaini mkataba wa mwaka mmoja tu na timu hiyo, hivyo baada ya msimu huu kumalizika yeye ni mchezaji huru.

“Pia kutokana na hali ilivyo kwake hawezi kuwa na mshahara mkubwa kama Mayele kwa kuwa anahitaji zaidi timu ya kuchezea kwa sasa na atakuwa na nafasi ya kucheza timu kubwa zaidi kuliko kushuka ligi ya Motsepe Foundation Championship,” liliendelea kuandika.

Hata hivyo, pamoja na gazeti hilo halijasema Chivaviro alikuwa anachukua mshahara kiasi gani akiwa na Marumo, ila inafahamika ni zaidi ya milioni 15 kwa mwezi, akiwa ana uzoefu mdogo kwenye ligi hiyo.

Staa huyo jumla alifanikiwa kufunga mabao 17 msimu mzima, huku Mayele hadi sasa akiwa na mabao 33, akiwa na nafasi ya kuongeza mengine wakati watakapovaana na USM Alger Jumamosi, mechi mbili za Ligi Kuu Bara pamoja na fainali ya Azam Federation baadaye mwezi ujao.

SOMA NA HII  ALICHOSEMA MANARA KUHUSU MCHANGO WA RAIS SAMIA KWENYE MECHI YA JUZI...ATAJA MILION 41..