Home Habari za michezo BAADA YA KUMALIZANA NA AFCON…NOVATUS ATUA MARSEILLE YA LIGI KUU UFARANSA…

BAADA YA KUMALIZANA NA AFCON…NOVATUS ATUA MARSEILLE YA LIGI KUU UFARANSA…

Habari za Michezo

MAANDALIZI ya miamba ya soka la Ukraine, Shakhtar Donetsk yameendelea kuiva huku kiungo wa kimataifa wa Tanzania, Novatus Dismas akiwa sehemu ya chama hilo ambalo linakibarua cha kucheza dhidi ya Marseille kwenye michuano ya Europa League, Alhamisi ya Februari 15.

Novatus alipewa dakika 90 kwenye mchezo wa kirafiki dhidi ya Velez Mostar ili kuwa fiti kwa ajili ya kuivaa Marseille inayonolewa na nyota wa zamani wa AC Milan na timu ya taifa la Italia, Gennaro Gattuso.

Mchezo huo wa kirafiki ulikuwa wa tatu kwa Shakhtar, Novatus hakuwepo kwenye michezo miwili iliyopita kutokana na kuwa kwake sehemu ya kikosi cha Taifa Stars kwenye Fainali za Mataifa ya Afrika 2023.

Shakhtar imeangukia Europa League baada ya kushindwa kumaliza katika nafasi mbili za juu kwenye msimamo wa kundi H la Ligi ya Mabingwa Ulaya hivyo kumaliza kwao nafasi ya tatu kuliwafanya kuwa na sifa za kucheza hatua ya mtoano kwenye michuano hiyo.

Katika michezo ya hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, Novatus alipata nafasi ya kucheza mchezo mmoja tu akiwa na miamba hiyo na kuwa Mtanzania wa pili kucheza michuano hiyo mikubwa zaidi Ulaya katika ngazi ya klabu nyuma ya Mbwana Samatta.

Upande wa Europa League napo anafuata nyayo za Samatta ambaye alicheza michuano hiyo akiwa na KRC Genk, nahodha huyo wa Taifa Stars ndiye mchezaji pekee wa Kitanzania aliyecheza michuano yote mikubwa ya Ulaya na sasa anakiwasha kwenye Europa Conference League.

SOMA NA HII  MANULA KURUDI AZAM FC..?... UKWELI WOTE UNAOPASWA KUJUA HUU HAPA...