Home Habari za michezo KISA KUBANIWA NA AZAM FC…KAPOMBE KAIBUKA NA HILI JIPYA SIMBA…

KISA KUBANIWA NA AZAM FC…KAPOMBE KAIBUKA NA HILI JIPYA SIMBA…

Habari za Simba leo

Baada ya kutokidhi matarajio ya mashabiki wao katika mchezo wa Dabi ya Mzizima ulipigwa juzi katika Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, beki wa Simba, Shomari Kapombe amewatuliza mashabiki hao na kuwaomba waungane kwa ajili ya kupata ushindi katika mchezo wa kesho dhidi ya Geita Gold, huku akiahidi kwamba wachezaji wamejifunza na watapambana kuwapa furaha.

Simba nusura iangushe pointi tatu juzi mbele ya Azam FC kabla ya Clatous Chama kuinusuru kwa kusawazisha bao dakika ya 90 baada ya Azam FC kutangulia mapema kwa bao la dakika ya 14 lililofungwa na Prince Dube na kufanya dabi hiyo ya kwanza kuchezwa Uwanja wa CCM Kirumba jijini kumalizika kwa sare na kuendelea kuipa Yanga uhakika wa kukaa kileleni wa msimamo wa Ligi Kuu na pointi zao 37.

Kesho Simba itakuwa tena uwanjani hapo kumenyana na Geita Gold kuanzia saa 10:00 jioni kumalizia mchezo wake wa nne Kanda ya Ziwa baada ya Mashujaa, Tabora United na Azam FC, hata hivyo, Simba inaingia kwenye mchezo huo ikiwa na jeuri kubwa kwani mchezo wa msimu uliopita uliozikutanisha timu hizo katika Uwanja wa CCM Kirumba, Mnyama alipata ushindi mnono wa mabao 5-0.

Akizungumza jijini hapa baada ya sare hiyo, Kapombe amesema kwamba lengo lao katika mchezo huo lilikuwa kuwafurahisha mashabiki wao kwa kuendelea kuvuna pointi tatu lakini Azam waliwatibulia baada ya kukutana na mchezo mgumu tofauti na matarajio yalivyokuwa.

Amesema kikosi chao kimejifunza kwa kilichotokea juzi na sasa wanajipanga kwa mchezo wa kesho ambao wamedhamiria kuvuna ushindi na kupata alama tatu zitakazoendelea kuwapa matumaini ya kushindana kwenye mbio za ubingwa wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Azam na Yanga.

“Tunashukuru Mwenyezi Mungu mchezo uliisha salama tumeweza kupata pointi moja hayakuwa matarajio yetu maana sisi tulijipanga kupata alama tatu lakini tunashukuru Mungu kwa hiyo pointi moja, ukiangalia mchezo ulikuwa mgumu zaidi kwa sababu tumeruhusu bao la mapema kwa hiyo ikahitaji nguvu kubwa ya kuwezesha kusawazisha lakini tulisimama katika mstari ule ule wa mwalimu alichotuelekeza,” amesema.

“Na baadaye tukasawazisha na kupata pointi moja, mimi na wachezaji wenzangu naweza kusema mchezo huu tumeshaumaliza tumeweka pembeni sasa tuna-focus kwa ajili ya mchezo unaokuja tunakwenda kujipanga kwa ajili ya kupata pointi tatu tunajua hautakuwa mwepesi lakini tunakwenda kujipanga ili kupata pointi tatu.

“Tunawashukuru wana Mwanza kwa kuja kutusapoti katika mchezo wa leo na vilevile nawaomba waendelee kutusapoti na kuipa timu yao nguvu kwa ajili ya kupata ushindi katika mchezo unaokuja.”

Shabiki wa timu hiyo, Aggy Simba amesema kikosi chao kiliangushwa na uamuzi usio sahihi wa marefa, lakini mashabiki bado wana imani na wachezaji wao na wanaridhishwa kwa namna wanavyopambana, huku akitamba kuwa haijaisha kwani mchezo wa kesho wamedhamiria kuvuna pointi tatu.

SOMA NA HII  KWA KOCHA HUYU...SIMBA SASA VILIO BASI...STAILI YAKE YA SOKA KAMA LA BARCELONA..KUANZA NA RUVU SHOOTING..