Home Habari za michezo FUNZO LA UKIMYA ANAREJEA KAZINI, SINGANO

FUNZO LA UKIMYA ANAREJEA KAZINI, SINGANO

2
0

BAADA ya kimya kingi cha aliyekuwa winga wa Simba, Azam FC na TP Mazembe, Ramadhan Singano anasimulia kilichomuweka nje ya uwanja na utayari wake wa kurejea kazini kwa sasa.

Katika mahojiano baina yake na Mwanaspoti, Singano maarufu hapa nchini kwa jina la Messi anasema kuna funzo alilopata katika ukimya wake, hasa jinsi ya kuishi na jamii.

“Ukiwa unacheza, unatumia muda mfupi sana kushirikiana na jamii, lakini kwa muda niliokaa na jamii nimejua ina picha gani kunihusu,” anasema mchezaji huyo.

Anasema mastaa wanaotamba kwa sasa ni vizuri wakajua kuna maisha mengine yatakayotafsiri matendo yao ya sasa, hivyo anawashauri waache picha sahihi katika jamii.Anasimulia kilichokuwa nyuma ya ukimya wake kuwa ni masuala ya kimkataba baina yake na TP Mazembe aliyojiunga nayo msimu wa 2019/20 akitokea Azam FC.“Nilijiunga na TP Mazembe kwa mkataba wa miaka mitano. Ilikuwa 2019/20. Yapokuna mambo hayakwenda sawa baada ya wao kunitoa kwa mkopo kwenda Nkana ya Zambia mwaka 2021, hadi Fifa ikaingilia kati. Tayari tulishamalizana mwaka jana; nipo tayari kuendelea na maisha yangu mengine, kwa sasa nipo huru,” anasema.Je, anajuta kujiunga na TP Mazembe? Nyota huyo anafafanua hilo kwa maana mbili; ameondoka na funzo la namna klabu hiyo ilivyokuwa imewekeza na ushindani ulivyokuwa mkubwa, kwani mchezaji anayepata nafasi ya kucheza ni yule aliye na kiwango cha juu.“Tulijiunga TP Mazembe kipindi hicho walikuwepo wachezaji wenye majina makubwa Afrika, kama kipa Robert Kidiaba, hadi aliwahi kupewa Uwaziri wa Michezo wa DR Congo. Mtu kama huyo ujue alifanya makubwa hadi serikali ya nchi hiyo ikaona ana kitu cha kuchangia katika sekta hiyo.”

Anaongeza kuwa, “nilibahatika kukaa naye karibu, na alikuwa anatuona kama ndugu zake. Kwa kile ambacho Mbwana Samatta alikifanya, kiliacha alama ya Watanzania kuaminika. Kikubwa zaidi, nilijifunza uvumilivu na nidhamu kutoka kwake.

“Ushindani uliokuwepo ulinitafsiri thamani ya kiwango na upambanaji wangu nje ya nchi; hivyo katika hilo nilifaidika. Labda upande wa changamoto ni ukimya, kwani watu walikuwa hawajui nipo wapi na kwa nini, baada ya kutokea tofauti ya kimkataba baina yangu na wao.”

Anasema kitendo cha TP Mazembe kumtoa Nkana kwa mkopo kilitokana na shauku yake ya kupata timu ya kucheza, lakini changamoto ikawa ni ukiukwaji wa baadhi ya vipengele vilivyokuwapo katika mkataba, vikafanya ndoto yake iishie njiani na ikawa chanzo cha kurejea Tanzania.

“Isingekuwa changamoto hiyo, ningekuwa bado nipo uwanjani kama ambavyo wenzangu wanacheza, kama Seseme (Abdallah), Ndemla (Said), Mkude (Jonas) na wengine wengi. Ikitokea nafasi, nitarejea kukamilisha deni nililonalo la kuendelea kukitendea haki kipaji changu,” anasema.Anathibitisha zipo faida na hasara kwa mchezaji anayetaka kuendelea na ndoto za mpira wa miguu kufanya mazoezi nje ya timu kwa muda mrefu, kwani atakuwa anakosa kujiamini wakati wa mechi za mashindano.

“Sikuwahi kuacha kufanya programu ya mazoezi. Wakati mwingine nacheza mechi za mtaani ili kulinda kiwango changu, lakini huwezi kufananisha na wanaocheza Ligi Kuu, ambao muda wote wanajifunza mbinu za makocha na ushindani wa namba baina yao na timu pinzani,” anasema Singano, na kuongeza:

“Faida ni kwamba nimejifunza vitu vingi vya maisha nje ya kazi hiyo. Nimepata muda wa kusimamia miradi yangu ninayowekeza, na kuibua ndoto za wachezaji wengine kupitia kituo changu. Tayari kuna kipa anaitwa Daniel; kuna kituo kingine ambacho nimempeleka Mwanza.”

Singano anatamani siku zingerudi nyuma apate nafasi nyingine ya kufurahia maisha ya Simba B, walivyoishi kwa umoja, upendo na nguvu ya kuzipambania ndoto zao.

“Kiuchumi nitasimulia Simba ya wakubwa, maana zipo baadhi ya hatua nilizozipiga, ila maisha nisiyoyasahau ni ya Simba B. Tulijengwa katika upambanaji na upendo; hadi sasa tunawasiliana na kutafutana. Natamani itokee nafasi nyingine yajirudie,” anasema Singano, na kuongeza:

“Tulikuwa tunatamani ile Simba B ihamishwe, wachezaji wote waende timu moja halafu tukakabiliane na wapinzani. Ukiachana na sisi ambao tulijulikana kama Hassan Isihaka, Said Ndemla, Abdallah Seseme, Jonas Mkude na Edward Christopher, wapo wengine wengi waliokuwa na vipaji vikubwa mno.”

Mbali na hilo, amekiri kujifunza kitu kikubwa katika uhamisho wake wa kutoka Simba aliyojiunga nayo mwaka 2011 na kutua Azam mwaka 2015: “Nilijifunza utulivu na ukimya, kwa sababu maneno yalikuwa mengi; mashabiki baadhi hawakunielewa, lakini maisha ya mchezaji ndivyo yalivyo.”

Anaongeza: “Ndiyo maana hata nilipopata changamoto na TP Mazembe, hakuwahi kusikia nikizungumza popote; nilikaa kimya. Ukicheza timu iliyo na mashabiki halafu ukapendwa, ikitokea unahama wanakuona kama msaliti. Sasa hapo ilikuwa Simba kwenda Azam; vipi ingekuwa Simba kwenda Yanga, au mchezaji aliyeko Yanga kwenda Simba? Lazima atapata changamoto ya kuchukiwa. Jambo la msingi ni wajifunze kukaa kimya.”

Anasema maisha ya Azam yalikuwa mazuri na yalimfungulia milango ya kwenda kujifunza soka la kimataifa: “Nilitokea Azam kwenda TP Mazembe, kisha Nkana. Pia zipo hatua za kiuchumi nilizozipiga kwa kile ambacho nilikipata, ingawa sitaweza kutaja kitu kimoja baada ya kingine.”

Anasema ingawa akiangalia Ligi Kuu anaviona vipaji vikubwa na ushindani, inakuwa ngumu kwake kueleza anatamani kucheza na nani hadi apate nafasi ya kuingia uwanjani na kuuona uhalisia, tofauti na aliowahi kufurahi kucheza nao kipindi cha nyuma.

“Nilikuwa nikicheza na kaka zangu kama Haruna Moshi ‘Boban’, Amri Kiemba, na wenzangu wengine Seseme na Salum Abubakar ‘Sure Boy’. Nilikuwa nanaf urahia, kwani ni mafundi, ila wapo wengi; kwa kifupi hao ni baadhi,” anasisitiza, akisema aliyekuwa anamkubali tangu akiwa mtoto ni Boban.Anasema vitu ambavyo hatakaa avisahau ni kupandishwa kutoka timu B kwenda Simba A. Uchungu alioupata ni kukosa mishahara ya miezi mitatu: “Baada ya kupanda, nikatamani niachane na soka. Kaka zangu walisema napaswa kuongeza bidii nitaanza kufurahia kipaji changu, na maneno yao yalitimia baada ya kuyazingatia. Jambo lingine nilipata nafasi ya kuitumikia Taifa Stars.”

Anasema nje ya mpira wa miguu anapendelea kusoma vitabu vyenye mafunzo, akikitaja kimojawapo kuwa ni Watoto wa Mama Ntilie, kilichojaa mafunzo ya kweli ya mtaani.

“Watu tulikotokea maisha ya chini, hicho kitabu ukikisoma kina funzo, tofauti na watoto wa ushuani. Napenda kusoma vitabu mbalimbali ili kupanua uwezo wa kufikiri na kutafsiri vitu katika jamii,” anasema.

Singano anakumbuka akiwa mdogo alikuwa akienda na wenzake majalalani kuokota mkaa; kisha akiukusanya mwingi anapeleka nyumbani. Wakati mwingine anauza ili kupata fedha ya kujikimu au kumpa mama yake mzazi kusaidia nyumbani.

“Tunaenda ambako gari la mkaa limeshuka, tunaokota uliobaki; wakati mwingine mpaka majalalani. Kifupi, nimepitia mengi, lakini nashukuru Mungu hapa nilipo sasa haikuwa rahisi hadi Watanzania kunifahamu. Jambo ninalolitamani ni wazazi wangu wangekuwa hai, wangekula kidogo nilichokipata,” anasema Singano, akiwa mtoto wa mwisho kati ya sita; kaka zake wakiwa ni Khamis, Moghammed na Bakari, huku wawili wakitangulia mbele ya haki.