Mshambuliaji wa Pyramids FC ya Misri, Fiston Mayele ametembelea hoteli iliyoweka kambi Simba SC, katika Jiji la Cairo nchini Misri.
Nyota huyo wa zamani wa Yanga SC alipowasili kambini hapo, amelakiwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, Salim Abdallah ‘Try Again’, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally pamoja na nyota wa klabu hiyo, Fabrice Ngoma.
Kesho saa 5:00 usiku, wababe hao wa mitaa ya Msimbazi na Kariakoo watashuka dimbani kwaajili ya mchezo wa marudiano wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL) dhidi ya mabingwa wa nchini humo Al Ahly hapo kesho saa 5:00 usiku.
Katika hatua nyingine, Klabu ya soka ya Al Ahly imeifanyia umafia Simba Sc baada ya kuwasili nchini Misri kwa ajili ya mchezo wa marudiano wa robo fainali ya CAFCL utakaopigwa kesho Ijumaa nchini humo.
Mwandishi wa habari wa Clouds Media ambaye yupo kwenye msafara wa Simba ulioenda Cairo Misri kwa ajili ya mchezo huo, ameshuhudia tukio hilo na hapa anasimulia.
“Al-Ahly kupitia Rider walifanya uhuni wa kulizungusha basi la wachezaji wa Simba kwa dakika (45′) kwenda Hotelini sehemu ya dakika (10′) .. Mwenyekiti wa bodi ya Simba, Salim Abdallah ‘Try again’ ikamlazimu kupambana na askari aliyekuwa anaongoza Rider ambaye baadae akasema yalikuwa ni maagizo kutoka Al-Ahly,” amesema Nassib Mkomwa.