Home Habari za michezo MAISHA YA KIFAHARI YA PEP GUARDIOLA NA UTAJIRI WA SH280 BILIONI

MAISHA YA KIFAHARI YA PEP GUARDIOLA NA UTAJIRI WA SH280 BILIONI

0

KOCHA wa Manchester City, Pep Guardiola anaishi kibosi sana. Tangu apate jina akiwa na Barcelona, Bayern Munich na sasa Man City, amevuna pesa za kutosha pamoja na mafanikio makubwa ikiwamo kubeba mataji makubwa ya ligi na Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Kwenye pesa ni mmoja wa makocha wanaolipwa pesa nyingi na hivyo akiwa anafikiria hatma yake Man City, hata akiacha kazi kabisa maisha yake bado yataendelea kwenda kutokana na utajiri alionao.

ANAVYOPIGA HELA

Guardiola analipwa mshahara mkubwa Manchester City unaokadiriwa kufikia kati ya Pauni milioni 20 hadi 23 kwa mwaka (sawa na zaidi ya Sh65 bilioni). Hii inamfanya kuwa mmoja wa makocha wanaolipwa zaidi duniani.

Mbali na mshahara huo, hupata bonasi nono kutokana na mafanikio ya timu. Kwa mfano, kutwaa Ligi Kuu England au Ligi ya Mabingwa Ulaya kunaweza kumuingizia mamilioni ya pauni za ziada. Pia ana mikataba ya matangazo na ushirikiano na kampuni mbalimbali, zikiwamo Nike na Nissan zinazoongeza kipato chake kwa kiasi kikubwa kila mwaka.

Kocha huyo amejijengea utajiri mkubwa kupitia mafanikio yake kama kocha, akiwa na makadirio ya utajiri wa karibu Pauni 100 milioni (zaidi ya Sh280 bilioni).

ANAVYOTUMIA HELA

Licha ya kipato kikubwa, Guardiola anajulikana kwa matumizi yenye mpangilio. Anawekeza zaidi katika mali zisizohamishika kama nyumba na biashara ndogo ndogo. Pia hutumia fedha kwa safari, mapumziko na maisha ya kifahari, lakini si kwa fujo kama mastaa wengine wa soka.

Anaaminika kutumia fedha nyingi katika elimu ya watoto wake na kusaidia shughuli za kijamii, jambo linaloonyesha anaangalia zaidi mustakabali wa familia kuliko anasa pekee.

MAGARI ANAYOMILIKI NA THAMANI ZAKE

Audi RS6 Avant – Pauni 100,000

Bentley GTX700 – Pauni 250,000

Mercedes-Benz GLE –Pauni 70,000

Range Rover Vogue – Pauni 100,000

NYUMBA

Guardiola anamiliki nyumba kadhaa katika maeneo tofauti, ikiwamo England na Hispania. Nyumba zake zina thamani ya mamilioni ya pauni, zikiwa na miundombinu ya kisasa kama mabwawa ya kuogelea, bustani kubwa na usalama wa hali ya juu.

Nyumba yake ya Manchester iko katika eneo la kifahari yenye thamani ya Pauni 11 milioni, huku pia akiwa na nyingine Barcelona, Hispania, katika eneo la Pedralbes, ambalo ni la matajiri linalokadiriwa kuwa na thamani Pauni 7 milioni.

MISAADA KWA JAMII

Kocha huyu hajisahau linapokuja suala la kusaidia jamii. Amechangia fedha katika sekta ya afya, hasa wakati wa janga la COVID-19 nchini Hispania. Pia amekuwa akisaidia miradi ya watoto na elimu.

Zaidi ya hapo, Guardiola amekuwa akitoa sauti yake katika masuala ya kijamii na haki za binadamu, akionesha kuwa mafanikio yake hayaishii uwanjani pekee.

MAISHA YA FAMILIA

Guardiola na Cristina Serra walifunga ndoa mwaka 2014 baada ya kuwa pamoja kwa zaidi ya miaka 20 na walikutana wakiwa vijana, Pep akiwa na miaka 18 na wana watoto watatu: Maria, Màrius na Valentina.

Kwa mujibu wa taarifa za hivi karibuni, Pep na Cristina walitengana mwaka 2024/2025 baada ya kuwa pamoja kwa zaidi ya miaka 30, ingawa wanaendelea kuwa na mahusiano mazuri kwa ajili ya familia yao.