Home Habari za michezo CLARA LUVANGA ATIKISA SOKO LA USAJILI SAUDI ARABIA

CLARA LUVANGA ATIKISA SOKO LA USAJILI SAUDI ARABIA

0

KUTOKANA na kiwango anachoendelea kuonyesha mshambuliaji wa Kitanzania, Clara Luvanga anayekipiga Al Nassr ya Saudi Arabia, kimeifanya menejimenti yake kutamba.

Mkataba wa nyota huyo unatarajiwa kumalizika Juni 30 mwaka huu, hali inayozifanya klabu mbalimbali kuanza kuangalia uwezekano wa kumnasa, huku menejimenti yake ikiendelea kuchambua ofa zitakazoendana na thamani yake.

Taarifa kutoka karibu na mchezaji huyo zinaeleza, ili Clara aendelee kubaki Al Nassr au kujiunga na timu nyingine, uhamisho wake lazima uwe kwenye kiwango cha kuanzia Sh90 milioni hadi 100 kwa mwaka.

Kwa sasa mshambuliaji huyo amekuwa mhimili muhimu katika kikosi hicho kutokana na uwezo wake wa kufunga na kuibeba timu katika mechi muhimu, jambo linaloongeza thamani yake.

Msimu huu alimaliza akiwa mfungaji bora wa ligi hiyo akiweka kambani mabao 24, msimu wake wa kwanza 2023/24 alifunga mabao 11 na asisti saba wakati uliofuata aliweka kambani mabao 21 na asisti saba.

Inaelezwa Al Nassr ipo kwenye mazungumzo ya kuongeza mkataba wake, lakini uamuzi wa mwisho utategemea kama wataweza kukidhi matakwa ya kifedha ya upande wa mchezaji huyo.

Chanzo hicho kinasema Clara yupo tayari kubaki Al Nassr iwapo ataongezewa masilahi yanayolingana na mchango wake, pia yuko wazi kupokea ofa kutoka klabu nyingine mradi tu ‘maokoto’ yawe mazuri zaidi.

“Ana Ofa nyingi sana ila kwa sasa atakachokiangalia ni pesa kwanza na sio kingine. Kwa hiyo hata kama timu ipo India ila ina pesa kuwazidi wote waliomuwekea ofa, ataenda,” kimesema chanzo hicho.

Uhamisho wa Clara kutoka Dux Lugrono ya Hispania kwenda Al Nassr uligharimu kiasi cha Sh51 milioni ya usajili, lakini mshahara wake ndani ya misimu mitatu, mwaka wa kwanza  alikunja sh19 milioni, mwaka jana alilipwa sh23 milioni na mwaka huu analipwa sh27 milioni.