HII ndiyo sababu ya Yanga SC kuendelea kuwa timu bora Tanzania na kudumisha rekodi ya kutopoteza mechi kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara.
Kocha Mkuu wa Yanga, Pedro Goncalves, ameweka wazi kuwa nidhamu na kuheshimu mpinzani ndio silaha yao kuu, hata baada ya mchezo mgumu wa Kariakoo Derby dhidi ya Simba SC uliomalizika kwa sare ya 2-2.
Goncalves hakukwepa ukweli kuhusu makosa yaliyofanywa na wachezaji wake na amekiri wazi kuwa timu yake ilikuwa na mwanzo mbaya, jambo lililowapa wapinzani nafasi ya kufunga mabao mawili ya mapema.
“Tulikuwa na mwanzo mbaya. Tulionyesha udhaifu kwenye dakika za kwanza,” alisema kocha huyo.
Hata hivyo, amesisitiza kuwa pamoja na udhaifu huo, kiujumla Yanga ilicheza mpira bora zaidi na ilistahili kuondoka na alama tatu.
“Tulikuwa bora kuliko Simba na tulistahili ushindi,” aliongeza Pedro. Alipongeza juhudi za wachezaji wake walioonyesha moyo wa kupambana na kusawazisha baada ya kuwa nyuma kwa 2-0, akisema hilo ndilo jambo linaloifanya Yanga kuwa tofauti.
Kuhusu mabadiliko ya kuwaingiza Kouassi Attohoula Yao na Laurindo Dilson Maria Aurelio ‘Depu’ kipindi cha pili, Goncalves alikanusha kuwa ilikuwa papatiko la ghafla.
Amefafanu kuwa mabadiliko hayo yalikuwa sehemu ya mikakati yao tangu mwanzo wa mchezo, si shinikizo la matokeo.
“Hakuna sababu nyingine, Sikulazimika kubadilisha kwa presha, Ilikuwa sehemu ya mipango yetu ili kuondoka na alama, na tumefanikiwa kupata moja,” amesisitiza.
Kauli ya Pedro inaonyesha wazi falsafa ya Yanga, kukubali makosa, kuheshimu wapinzani ba kuamini mchakato.
Ni nidhamu hii inayoiweka Wananchi kileleni mwa soka la Tanzania, wakibeba matumaini ya mashabiki wao kila wanapoingia uwanjani.