Habari za michezo

MICHAEL OLISE HAT TRICK YA MAANA

Vardo June 9, 2026 2:29 pm

LILLE, UFARANSA: KIUNGO mshambuliaji wa Ufaransa Michael Olise ameendelea kuonyesha kiwango chake bora kuelekea Kombe la Dunia baada ya kufunga mabao matatu (hat-trick) na kuiongoza Ufaransa kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Northern Ireland katika mchezo wa kirafiki uliochezwa mjini Lille, jana.

Olise, ambaye amekuwa katika kiwango cha juu katika miezi ya hivi karibuni, ameendelea kujidhihirisha kama moja ya silaha muhimu za safu ya ushambuliaji ya kikosi cha Ufaransa. Hata hivyo, pamoja na ushindi huo, maswali kuhusu uimara wa safu ya ulinzi ya Les Bleus bado yanaendelea kuibuka, siku nne baada ya kupoteza kwa mabao 2-1 dhidi ya Ivory Coast.

Ufaransa itaanza kampeni yake ya Kombe la Dunia Juni 16 kwa kucheza dhidi ya Senegal katika Kundi I, kabla ya kukutana na Iraq na Norway.

Kocha Didier Deschamps aliwatumia nyota wengi wanaotarajiwa kuanza katika mchezo wa ufunguzi, huku Olise akiungana na Kylian Mbappe, Ousmane Dembele na Desire Doue katika safu ya ushambuliaji. Katikati ya ulinzi walikuwepo William Saliba na Dayot Upamecano.

Ufaransa ilianza mchezo kwa kusuasua huku ikishindwa kwa muda mrefu kupenya ukuta wa ulinzi wa wapinzani. Hata hivyo, dakika mbili kabla ya mapumziko walipata bao la kuongoza baada ya Doue kufanya kazi nzuri upande wa kushoto na kumtafuta Dembele ndani ya eneo la hatari. Shuti la mshambuliaji huyo lilipanguliwa na kumkuta Olise aliyefunga kwa urahisi.

Dakika nne baada ya kipindi cha pili kuanza, Olise aliongeza bao la pili kwa shuti kali la voli kufuatia kuondolewa vibaya kwa mpira na mabeki wa Ireland.

Pamoja na ubora wao mbele ya lango, Ufaransa walionekana kuyumba mara kadhaa nyuma na walijikuta wakiruhusu mashambulizi ya kushtukiza. Hali hiyo iliwapa wageni bao la kufutia machozi kupitia Patrick Kelly aliyemalizia kwa nguvu krosi ya Shea Charles.

Lakini nyota wa mchezo alikuwa Olise.

Katika dakika ya 75, mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 24 alikamilisha hat-trick yake kwa shuti la kuvutia lililokwenda moja kwa moja kona ya mbali ya lango, na kuhitimisha ushindi wa mabao 3-1 kwa Ufaransa.

Kwa kiwango anachoendelea kukionyesha, Olise anaonekana kuwa miongoni mwa wachezaji watakaobeba matumaini makubwa ya Ufaransa katika harakati za kusaka ubingwa wa Kombe la Dunia.

JANGWANI KUMENOGA YANGA KUMALIZANA NA MSHAMBULIAJI HATARI GIZA ISHU YA CHRISTIAN ERIKSEN KUSTAAFU