Riyad Mahrez Atundika Daluga
DALLAS, MAREKANI: MKONGWE Riyad Mahrez ametangaza kustaafu kuchezea timu ya taifa dakika chache baada ya Algeria kutolewa kwenye Kombe la Dunia.
Nyota huyo wa zamani wa Manchester City na Leicester City, Mahrez, alishuhudia Algeria ikiondolewa baada ya kufungwa mabao 2-0 na Uswisi leo Ijumaa.
Baada ya mechi, winga huyo mwenye umri wa miaka 35 alitangaza kuwa huo ulikuwa mchezo wake wa mwisho akiwa na timu ya taifa ya Algeria.
Mahrez, ambaye ameshinda taji la Ligi Kuu ya England mara tano, alitolewa uwanjani kipindi cha pili zikiwa zimesalia dakika 20 kumalizika kwa mchezo.
Algeria haikuonekana kuwa na uwezo wa kurejea mchezoni baada ya kuruhusu bao la mapema lililofungwa na Breel Embolo akiwa karibu na lango.
Mahrez aliyekuwa na hisia kali aliwapigia makofi mashabiki alipokuwa akitoka uwanjani, na pia aliwafuata kuwashukuru baada ya mchezo kumalizika.
Alifunga mabao mawili katika sare ya 3-3 dhidi ya Austria, matokeo yaliyosaidia Algeria na Austria kufuzu hatua ya 32 bora.
Hata hivyo, timu zote mbili zimeshindwa kuvuka hatua ya kwanza ya mtoano, na hivyo Mahrez akahitimisha safari yake ya miaka 12 na Algeria bila shamrashamra nyingi. Kwa ujumla, aliichezea Algeria mechi 119, akafunga mabao 40, na kusaidia timu hiyo kutwaa Kombe la Mataifa ya Afrika 2019 (AFCON).
Katika mahojiano ya baada ya mechi na beIN Sports, Mahrez alisema kwa huzuni kuwa ameamua kustaafu kuchezea timu ya taifa. Alionekana kuvunjika moyo alipokuwa akitoa tangazo hilo.
Kwa sasa Mahrez anacheza nchini Saudi Arabia akiwa na Al-Ahli, ambapo tayari amecheza zaidi ya mechi 120 na kufunga mabao 37.
Katika Ligi Kuu ya England, alicheza zaidi ya mechi 280 akiwa na Manchester City na Leicester City. Leicester ilimsajili kwa ada ya pauni 450,000 mwezi Januari 2014, na akajizolea umaarufu mkubwa msimu wa 2015/16 aliposaidia Leicester kutwaa ubingwa wa ligi kwa kishindo cha kushtua wengi.
Msimu huo alichaguliwa katika Timu Bora ya Mwaka, na pia akashinda tuzo za Mchezaji Bora wa Mwaka wa Wachezaji na Mchezaji Bora wa Mwaka wa Mashabiki baada ya kufunga mabao 17.
Manchester City baadaye ilimsajili mwaka 2018 kwa pauni60 milioni, na Mahrez akaendelea kushinda mataji makubwa 10 akiwa Etihad, yak iwemo yale ya kikosi kilichotwaa Treble msimu wa 2022/23.