Home Habari za michezo DANTE – MAYELE ANGENIUA JAMANI…MFUPA ULIKUWA UNAWAKA MOTO…AFUNGUKA ALICHOKIONA…

DANTE – MAYELE ANGENIUA JAMANI…MFUPA ULIKUWA UNAWAKA MOTO…AFUNGUKA ALICHOKIONA…


BEKI kisiki wa KMC, Andrew Vincent ‘Dante’ juzi aliruhusiwa kutoka hospitalini kisha akarudi tena jana kwa uangalizi zaidi baada ya kuumia kwenye mchezo wa timu yake na Yanga, lakini akafunguka kwa mara ya kwanza kwamba kama asingekuwa kuwa na mazoezi ya kutosha huenda straika Fiston Mayele angemuharibia maisha yake.

Dante hakumaliza dakika 45 za kwanza katika mchezo wao dhidi ya Yanga ni baada ya kuumia katika dakika ya 44 na kutolewa kabla ya kuwahishwa hospitali ya Rufaa ya Temeke kwa matibabu zaidi.

Akizungumza jana, Dante alisema tukio la kuumia kwake mpaka sasa hajajua aligongwa na kipi kutoka kwa Mayele kwamba kilikuwa ni kiwiko cha mkono au goti la mshambuliaji huyo.

Dante alisema alipogongana na mshambuliaji huyo alipambana kuendelea na mchezo, lakini kadri ya muda ulivyosogea alianza kusikia maumivu makali zaidi na kuamua kukaa chini ambapo baadaye yaliendelea kuzidi.

“Pale uwanjani nilipatiwa matibabu lakini baada ya muda nikaona yale maumivu yanazidi tu na palikuwa panauma kweli mpaka nataka kulia,” alisema Dante aliyewahi kuichezea Mtibwa Sugar na Yanga na kuongeza;

“Sijui mpaka sasa alinigonga na nini, ila ninachokumbuka ni Mayele ambaye alinigonga wakati anaukimbilia mpira na kama isingekuwa na mazoezi ya kutosha angeniumiza vibaya sana, hapa kiunoni nilikuwa naona kama ule mfupa wa chini ya mbavu kiunoni kama unawaka moto.”

Alisema alipofika hospitali alipigwa picha ya mionzi na kukutwa hajavunjika lakini maumivu yalikuwa makali ambapo jana tena alirudi hapo kwa kupigwa picha nyingine.

SOMA NA HII  KUHUSU UFUNGAJI BORA MSIMU HUU...MAYELE AZIDI KUMTAMBIA MPOLE...."SIKUBALI KIRAHISI"...