Kocha Mkuu wa Singida Big Stars Hans Van Pluijm, ametoa sababu ya kikosi chake kukubali kupoteza mchezo wa Mzunguuko wa 22 wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Wekundu wa Msimbazi.
Miamba hiyo ilikutana jana Ijumaa (Februari 03), Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam, na wenyeji kupata ushindi wa 3-1, yakifungwa na Jean Baleke, Saido Ntibazonkiza na Pape Sakho, huku bao la wageni likifungwa na Bruno Barosso.
Kocha Hans amesema kikosi chake kilipoteza mchezo huo, kutokana na kushindwa kuzimudu mbinu za Wapinzani wake, ambayo ilionekana kuwa bora dhidi yao.
Amesema Simba SC walionesha kiwango cha tofauti na ilivyozoeleka tangu msimu huu ulipoanza, hivyo iliku vigumu kwa wachezaji wake kwenda sambamba na kasi yao.
“Tumefungwa na Simba SC, jana ilikuwa bora sana , ilicheza mpira tofauti na vile ilicheza tangu ligi ianze Simba walicheza mpira bora kuwahi kuona katika Ligi ya Tanzania Bara nilifurahi kwani mpira mzuri unaifanya Ligi kuwa Bora”
“Yote kwa yote mchezo ulimalizika kwa amani Singida, tulizidiwa kiujumla kutokana na aina ya wachezaji walionao , kuwa na ubora” amesema Hans van Der Pluijm
Wakati huo huo Kocha Hans amesema kwa mpira uliochezwa na Simba SC jana Ijumaa, anaimani kila kocha wa Ligi Kuu Tanzania Bara angetamani kuifundisha Simba SC.