Home Habari za michezo KWA BALAA HILI LA MPANZU HUKO SIMBA….BALUA AJITAFAKARI AISEEE….

KWA BALAA HILI LA MPANZU HUKO SIMBA….BALUA AJITAFAKARI AISEEE….

Habari za Simba leo

EDWIN Balua alikuwa miongoni mwa wachezaji waliotarajiwa kung’ara ndani ya kikosi cha Simba SC msimu huu, hasa baada ya kuonyesha kiwango bora chini ya Juma Mgunda mwishoni mwa msimu uliopita 2023/24.

Uwezo wake wa kucheza nafasi tofauti kwenye safu ya ushambuliaji ulimfanya awe mmoja wa wachezaji waliokuwa na nafasi nzuri ya kuendelea kung’ara. Hata hivyo, mabadiliko ya mfumo wa uchezaji chini ya Fadlu Davids pamoja na usajili wa Elie Mpanzu katika dirisha dogo vimefanya Balua kupata kibarua kigumu cha kupata nafasi ya kucheza mara kwa mara.

Kwa mujibu wa takwimu za msimu huu, Balua amecheza jumla ya mechi nane (8) tu za Ligi Kuu Bara kati ya 21 na kupata dakika 317 pekee, akifunga mabao mawili (2) bila kutoa asisti yoyote.

Kwa upande mwingine, Mpanzu, ambaye amejiunga na timu katika dirisha dogo, tayari amecheza mechi tisa (9), akikusanya dakika 695, akifunga mabao mawili (2) na kutoa asisti mbili (2).

Tofauti hii inadhihirisha kuwa Mpanzu ananafasi ya kucheza mara kwa mara na kushawishi benchi la ufundi zaidi ya Balua.

KIBARUA CHAKE

Mpanzu ameleta ushindani mpya kwenye kikosi cha Simba. Uwezo wake wa kucheza kama mshambuliaji au kiungo mshambuliaji umemfanya kuwa mchezaji mwenye faida kubwa kwa mfumo wa Fadlu Davids. Mpanzu siyo tu anafunga, bali pia anahusika katika uundaji wa mashambulizi, jambo ambalo limemfanya kuwa na thamani kubwa ndani ya kikosi.

Kwa takwimu, Mpanzu siyo tu kwamba ana idadi sawa ya mabao na Balua, lakini pia ametoa asisti mbili, jambo linaloonyesha kuwa anashiriki zaidi katika uchezeshaji wa timu kuliko Balua.

Sababu nyingine ni mfumo wa Fadlu unavyomnyima nafasi Balua. Mgunda alikuwa akimtumia Balua kama mshambuliaji wa pembeni mwenye uhuru wa kushambulia, lakini chini ya Fadlu, mfumo umebadilika.

Fadlu amekuwa akitegemea zaidi wachezaji wenye uwezo wa kuchangia katika ulinzi na kushambulia kwa uwiano sawa, jambo ambalo Mpanzu amelifanya vyema kuliko Balua.

Mfumo wa 4-2-3-1 unaotumiwa na Fadlu unahitaji wachezaji wa pembeni kuwa na uwezo wa kupandisha mashambulizi na kushuka kusaidia safu ya ulinzi.

Mpanzu ameonyesha kuwa na uwezo wa kutimiza majukumu haya vizuri, huku Balua akionekana kuwa mchezaji wa kushambulia zaidi bila kuwa na mchango mkubwa kwenye eneo la ulinzi.

Mbali na hilo, kuongezeka kwa wachezaji wa nafasi yake kama Mpanzu na wachezaji wengine wa kikosi kimesababisha Balua kupata muda mdogo wa kucheza, hali inayoweza kumfanya apoteze kabisa nafasi yake kama hatapambana kurudisha ubora wake.

NAFASI ANAYO

Pamoja na changamoto anazokutana nazo, Balua bado ana nafasi ya kurejea katika ubora wake na kupambana kushindania nafasi kikosini. Hata hivyo, kuna mambo muhimu anayohitaji kufanya ili kufanikisha hilo.

Kocha wa zamani wa Mtibwa Sugar na Gwambina, Mohamed Badru anasema Balua anatakiwa kubadilika katika staili yake ya uchezaji kulingana na mahitaji ya timu.

“Balua anahitaji kubadilisha mtindo wake wa uchezaji ili kuongeza mchango wake kwa timu. Anatakiwa kuwa mchezaji wa aina ya “box-to-box” ambaye anaweza kushambulia na wakati huo huo kusaidia kulinda.”

Mbali na hilo, Badru anasema ushindani ni jambo la kawaida, na mchezaji yeyote anaweza kupoteza nafasi yake kama hayupo katika kiwango bora. Hata hivyo, wachezaji wenye uwezo wa kustahimili presha na kujifunza kutoka kwa wenzao ndio wanaofanikiwa kurudi kwenye kiwango bora.

Balua anatakiwa kuchukulia ushindani huu kama changamoto chanya na kujifunza kutoka kwa Mpanzu ili kuwa mchezaji bora zaidi.

SOMA NA HII  KISA GOLI 5 ZA NTIBAZONKIZA JUZI....YANGA 'WAMKURUPUSHA' MAYELE...AANZA MAZOEZI UPYAA..