Home Habari za michezo BINGWA MUUNGANO CUP KUBEBA SH150 MILIONI

BINGWA MUUNGANO CUP KUBEBA SH150 MILIONI

0

BINGWA wa Kombe la Muungano 2026, atazawadiwa Sh150 milioni, zawadi ambayo ni mara tatu ya mashindano yaliyopita.

Katika mashindano ya mwaka jana, Yanga ambayo ilitwaa ubingwa huo, ilizawadiwa Sh50 milioni.

Mbali ya kuongezeka kwa zawadi ya mshindi wa kwanza, waandaaji wa mashindano hayo pia wameongeza zawadi ya mshindi wa pili na sasa atabeba Sh100 milioni baadala ya Sh30 milioni za awali.

Ongezeko hilo la zawadi ni sehemu ya mkakati mpana wa kufanya mashindano hayo kuwa na ushindani mkubwa zaidi pamoja na kuvutia kibiashara.

Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Zanzibar (ZFF), Ahmada Hussein Vuai, amesema maandalizi yote ya mashindano hayo yamekamilika.

Kwa mujibu wa ratiba ya mashindano hayo, mabingwa watetezi Yanga, wataanza kutetea taji lao kwa kucheza dhidi ya Muembe Makumbi katika mchezo wa ufunguzi utakaopigwa Jumanne ya Aprili 21, 2026, saa 1:00 usiku kwenye Uwanja wa New Amaan Complex, Unguja.

Mashindano hayo yanayofanyika Uwanja wa New Amaan Complex, yataendelea Aprili 22 na KVZ itakutana na Azam saa 1:15 usiku.

Aprili 23, mabingwa wa Zanzibar Mlandege watavaana na Singida Black Stars saa 10:15 jioni. Baadaye saa 2:15 usiku, Simba watamenyana na Mafunzo.

Michuano hiyo itachezwa kwa mfumo wa mtoano na washindi wa mechi nne za awali watafuzu hatua ya nusu fainali baada ya mapumziko ya siku moja.

Aprili 25, mshindi kati ya Yanga na Muembe Makumbi, atakutana na mshindi wa mechi kati ya KVZ na Azam.

Nusu fainali ya pili itachezwa Aprili 26, ikiwakutanisha mshindi wa Mlandege dhidi ya Singida Black Stars na mshindi wa Simba dhidi ya Mafunzo. Mechi zote za nusu fainali zitaanza saa 2:15 usiku.

Fainali itapigwa Aprili 29, saa 2:15 usiku na timu mbili zitakazofika hatua hiyo zitapambana kuwania ubingwa na kitita cha Sh150 milioni.