KIUNGO wa Yanga, Mudathir Yahya, atakosa mchezo muhimu wa Kariakoo Derby dhidi ya Simba utakaopigwa Mei 3, 2026, kufuatia adhabu iliyotolewa na Kamati ya Uendeshaji wa Ligi.
Mudathir amefungiwa kucheza mechi tatu pamoja na kutozwa faini ya shilingi milioni moja (1,000,000), baada ya kupatikana na hatia ya kumpiga kiwiko mchezaji wa Pamba Jiji FC, Ibrahim Abraham, katika mchezo wa ligi uliopita.
Adhabu hiyo ni pigo kwa kikosi cha Yanga ambacho kilikuwa kinamtegemea kiungo huyo katika mechi hiyo yenye ushindani mkubwa na hisia kali baina ya watani wa jadi.
Mbali na kuukosa mchezo wa Derby dhidi ya Simba, Mudathir pia hatakuwepo katika michezo mingine miwili ya ligi dhidi ya KMC FC pamoja na Coastal Union, hali inayoongeza changamoto kwa benchi la ufundi la Yanga.
Kutokuwepo kwake kunatarajiwa kuathiri mipango ya kocha, hasa katika eneo la kiungo ambapo Mudathir amekuwa mhimili muhimu kwa ubunifu na uthabiti wa timu hiyo msimu huu.
Hata hivyo, Yanga italazimika kupanga upya kikosi chake na kutafuta mbadala atakayeziba pengo lake, huku mashabiki wakisubiri kuona timu hiyo itakabiliana vipi na changamoto hiyo kuelekea michezo ijayo muhimu.