Nahodha wa Yanga SC, Bakari Mwamnyeto, amesisitiza kuwa kuvuna alama moja mbele ya Simba kwenye Kariakoo Derby haijawaondoa Wananchi kwenye safari yao ya kutetea taji la Ligi Kuu Tanzania Bara.
Mwamnyeto, ambaye alikuwa shujaa wa mchezo huo baada ya kufunga bao la kusawazisha, alizungumza baada ya pambano kali lililomalizika kwa sare ya 2-2 Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Mbweni.
Beki huyo alikiri kuwa ligi ya msimu huu ina ushindani mkubwa, jambo linalowalazimu kupambana kwa kila tone la jasho ili kuvuna alama muhimu kwenye kila mchezo.
“Licha ya kutoka sare na Simba, haijawatoa kwenye mstari wa malengo yetu ya kutetea ubingwa kwa mara nyingine,” alisema Mwamnyeto. Ameeleza kuwa mchezo ulikuwa mgumu, hasa baada ya Simba kutangulia kupata mabao.
Hata hivyo, alifichua kuwa maelekezo ya kocha kipindi cha mapumziko na utayari wa kisaikolojia wa wachezaji ndio ulibadili mwelekeo wa mchezo.
“Baada ya kurudi kipindi cha pili tulijipanga vizuri na kufanikiwa kusawazisha. Sisi kama wachezaji tulikuwa tayari tangu tukiwa Zanzibar, hivyo tulijua nini cha kufanya ndani ya uwanja,” ameongeza nahodha huyo.
Mwamnyeto amesema matokeo hayo yanaiweka Yanga katika nafasi nzuri kwenye mbio za ubingwa, wanaongoza kileleni kwa tofauti ya pointi tano mbele ya wapinzani wao, na akaahidi kuwa kikosi kitaendelea kujipanga kwa umakini mkubwa kuelekea michezo ijayo ya Ligi Kuu na Kombe la Shirikisho la CRDB.