Home Habari za michezo MAN UNITED VS LIVERPOOL, MAINOO AIMARISHA NAFASI YA LIGI YA MABINGWA

MAN UNITED VS LIVERPOOL, MAINOO AIMARISHA NAFASI YA LIGI YA MABINGWA

0

MANCHESTER, ENGLAND: LIGI Kuu England iliendelea mwishoni mwa wiki iliyopita, lakini kulikuwa na takwimu za ajabu katika kila mchezo uliopigwa, ingawa zile za Manchester Unide katika ushindi dhidi Liverpool wa mabao 3-2, huenda zilibeba sura mbili tofauti katika mashindano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao.

Man United walipata ushindi, ingawa sare ingetosha kuthibitisha nafasi yao ya Ligi ya Mabingwa, hivyo kwa namna fulani matokeo yasingekuwa na uzito mkubwa kama wangepata pointi moja, lakini namna walivyocheza kipindi cha kwanza ilionyesha siku ya kipekee, kwani walitangulia kuongoza, lakini wakaruhusu mabao mawili ‘chapchap’ kile cha pili, na iwapo wangekaza wangeshinda na kuivuka United.

Lakini Kobbie Mainoo alifunga dakika ya 77 na kuipatia United pointi zote tatu pamoja na kuwa ushindi wa kwanza wa katika mechi mbili dhidi ya Liverpool tangu 2015-16, huku tofauti ya pointi kwa sasa ikiwa sita zikiwa zimesalia mechi tatu. Matokeo hayo pia yanamaanisha kocha Michael Carrick ameifunga kila timu katika ‘Big Six’ tangu achukue nafasi ya ukocha, jambo litakaloongeza nafasi yake ya kubaki baada ya msimu wa 2025-26.

Kipindi cha kwanza cha mechi hakikuonyesha dalili za ugumu ambao ungehitajika kupata ushindi, lakini United walionekana kujiamini na kudhibiti mchezo tangu mwanzo. Hata hivyo, kukosekana kwa baadhi ya nyota wa Liverpool kama Mohamed Salah, Alisson Becker na wengine kulichangia kujiamini kwa United.

Pamoja na hayo, kocha Arne Slot bado alianza na kikosi chenye uzoefu, lakini hakikuweza kuwa tishio kubwa kipindi cha kwanza. United walipata bao la kwanza kupitia Matheus Cunha, huku la pili likifungwa na Benjamin Sesko na kipindi cha kwanza walikuwa na umiliki wa mpira wa asilimia 38.2 lakini waliongoza 2-0.

Hata hivyo, mambo yalibadilika kipindi cha pili. Dominik Szoboszlai alipunguza pengo baada ya kosa la Amad Diallo, kisha akahusika tena katika bao la kusawazisha lililofungwa na Cody Gakpo kufuatia kosa la Senne Lammens. Ndani ya dakika 10 za kipindi cha pili, United walikuwa wamepoteza uongozi, huku Liverpool wakianza kushambulia kwa nguvu zaidi.

Safu ya kiungo ya United ilionekana kupoteza umbo, huku Casemiro na Mainoo wakisogea mbele kupita kiasi na kuacha ulinzi wazi. Baadaye, United walirejea kwenye mchezo na Mainoo akafunga bao la ushindi baada ya mpira uliorejeshwa na Amad.

Ushindi huo ulionyesha uimara wa kisaikolojia licha ya kuyumba kwa muda, jambo ambalo linaleta sura ya pili ya kikosi hicho, kwamba Carrick anakijenga kisaikolojia zaidi kuliko kimbinu kwani wachezaji haohao ndio ambao makocha Ruben Amorim na Erik Ten Hag waliwatumia, lakini waliambulia patupu uwanjani.

Ingawa kiwango chao cha kubadilika-badilika kinaweza kumtia wasiwasi Carrick, ushindi ni muhimu kwa sasa kwani umewahakikisha nafasi ya Ligi ya Mabingwa.

TAKWIMU MUHIMU

Kufuatia mchezo huo, kiungo wa Liverpool, Dominik Szoboszlai sasa amefikisha mabao 13 na asisti 10, akiwa mchezaji wa tatu kufikisha mabao 10+ na pasi zamabao 10+ msimu huu, baada ya Rayan Cherki wa Manchester City na Jarrod Bowen anayekipiga West Ham United, ambako amekuwa mtamu zaidi katika mechi hizi za mwisho mwisho.

Tangu kuondoka kwa Ruben Amorim, hakuna aliyefunga zaidi ya Benjamin Sesko aliyetupia bao lake la tisa kwenye Ligi Kuu England msimu huu na kumfanya kuwa mojawapo wa maingizo bora zaidi kwenye mashindano hayo, lakini yasiyoangaliwa kwa jicho la tatu la kuzisaidia timu wanazozichezea kwa ubora.

Kwa upande wa Liverpool watakuwa wameruhusu mabao 17 kutokana na mipira ya kutenga (set-pieces) msimu huu ikiwa ni rekodi yao mbaya zaidi katika misimu zaidi ya 10 iliyopita, jambo ambalo linawalazimu kurudi mezani kutafuta mafundi wa kukabiliana na mipigo hiyoya hatari kutoka katika timu zingine ili yaje yawaasaidie, kwani kadri misimu inavyokwenda kuanzia ujao huenda mambo yakawa magumu zaidi kwao.

Na ni kutokana na hilo, limechangia pia kwa Liverpool kupoteza mechi ya 18 msimu huu katika mashindano yote, jambo ambalo pia linatilia walakini katika namna timu hiyo inavyojilinda chini ya nahodha Virgil van Dijk. Kwa Man United hiyo ilikuwa ni mechi ya nane ya ushindi nyumbani kati ya tisa za Carrick akiwa na Manchester United msimu huu kwenye mashindano ya Ligi Kuu England.

MATOKEO EPL MECHI ZA WIKIENDI

Brentford 3-0 West Ham United

Newcastle United  3-1 Brighton

Wolves 1-1 Sunderland

Arsenal 3-0 Fulham

Bournemouth 3-0 Crystal Palace

Aston Villa 1-2 Tottenham