Ushindi wao wa mabao 2-0 dhidi ya Valencia mwishoni mwa wiki, licha ya kufanya mabadiliko makubwa kikosini, umeonyesha kuwa wana kikosi kipana na uwezo wa kuhimili presha.
Atletico wanaingia kwenye mechi hii wakijua wazi kuwa sare haitoshi wanahitaji ushindi. Historia inaonyesha wanaweza kufanya hivyo, kwani wameshinda michezo sita kati ya saba ya nusu fainali za Ulaya walizocheza, ikiwemo dhidi ya Arsenal 2018 kwenye Europa League.
Lakini changamoto kubwa kwao ipo kwenye rekodi mbaya ya ugenini. Katika michezo yao 10 ya mwisho ugenini, wameshinda mitatu huku wakipoteza sita. Zaidi ya hapo, wamepoteza mechi tatu za ugenini za Ligi ya Mabingwa msimu huu zote dhidi ya timu za England.
Historia ya mechi kati yao pia inaipa nguvu Arsenal katika uwanja huu waliwahi kuichapa Atletico mabao 4-0 na kwa ujumla hawajapoteza katika michezo tisa ya karibuni dhidi ya timu za Hispania.
Kwa upande mwingine, Atletico wamepoteza mechi sita kati ya saba walizocheza nchini England takwimu ambazo zinaweza kuathiri morali yao kabla ya pambano hili kubwa.
MBINU NA VITA YA UFUNDI
Kiufundi huu ni mchezo wa mbinu kati ya falsafa mbili tofauti, Arsenal wanapendelea mpira wa kumiliki, wakitumia mfumo unaobadilika kati ya 4-3-3 na 3-2-5 wanaposhambulia. Hapa, mabeki wa pembeni hupanda juu, huku viungo wakijaza katikati ili kutengeneza nafasi na kuisukuma Atletico nyuma.
Kiungo kama Martin Odegaard anakuwa kiungo muhimu katika kuunganisha safu ya kati na ushambuliaji, wakati Bukayo Saka akitumia kasi na ubunifu wake pembeni kuvunja ngome ya wapinzani.
Arsenal pia hutegemea kukabia juu wanapopoteza mpira ili kuwanyima wapinzani muda wa kupanga mashambulizi.
Kwa upande wa Atletico, Simeone anajulikana kwa mfumo wake wa 4-4-2 wenye nidhamu kali ya kujilinda. Timu yake hupunguza nafasi kwa kucheza kwa mistari miwili iliyokaribiana, wakisubiri nafasi ya kufanya mashambulizi ya kushtukiza (counter-attacks).
Hapa ndipo hatari yao ilipo kwa kasi ya Alvarez na ubunifu wa Antoine Griezmann, Atletico wanaweza kuadhibu makosa madogo ya Arsenal. Pia mipira ya adhabu au kuona inaweza kuwa silaha muhimu kwao.
HALI YA VIKOSI
Kwa upande wa Arsenal, kuna matumaini makubwa ya kurejea kwa Martin Odegaard na Kai Havertz lakini Jurrien Timber na Mikel Merino wataendelea kukosekana kwenye kikosi hicho.
Kwa Atletico, Alvarez anatajwa kuwa fiti licha ya hofu ya awali ya majeraha na anatarajiwa kuongoza safu ya ushambuliaji ya timu hiyo.
Alvarez aliandika historia baada ya kuvunja rekodi ya Lionel Messi, kwa kuwa Muargentina aliyefikisha mabao 25 ya Ligi ya Mabingwa kwa haraka zaidi akifanya hivyo ndani ya michezo 41, wakati Messi alihitaji michezo 42 kufikia idadi hiyo.
Wachezaji kama Giuliano Simeone, Marcos Llorente, Alexander Sorloth na David Hancko walipumzishwa wikiendi iliyopita lakini Jose Gimenez bado yuko kwenye hatihati huku Pablo Barrios na Nico Gonzalez wakikosekana.