Home Habari za michezo JESSE DERRY APUNGUZA HOFU CHELSEA

JESSE DERRY APUNGUZA HOFU CHELSEA

0

KINDA wa Chelsea, Jesse Derry, ametuma ujumbe wa kuwatuliza mashabiki baada ya kupata jeraha la kichwa lililompelekea kulazwa hospitalini wakati wa mchezo dhidi ya Nottingham Forest.

Derry (18), ambaye alikuwa akicheza mechi yake ya kwanza ndani ya Stamford Bridge, alipoteza fahamu muda mfupi kabla ya mapumziko baada ya kugongana vichwa na mchezaji wa Forest, Zach Abbott.

Baada ya tukio hilo, alilazimika kutolewa nje ya uwanja kwa machela akiwa anapewa msaada wa oksijeni, hali iliyozua hofu kubwa uwanjani, hususan kwa baba yake, Shaun Derry, aliyekuwa na majonzi makubwa.

Licha ya Chelsea kukubali kichapo cha mabao 3-1, habari njema ni kwamba kijana huyo amepata nafuu na amewasiliana na mashabiki kupitia ukurasa wake wa Instagram.

Derry ametuma ujumbe akiwa bado anatibiwa hospitali ambao umeambatana na picha zake akiwa uwanjani ambapo ameandika: “Ni ndoto iliyotimia kuanza mchezo Stamford Bridge kwa mara ya kwanza kwenye mechi ya EPL. Ningependa kuwashukuru wafanyakazi wa matibabu wa Chelsea, kila mmoja katika hospitali ya St Mary’s, wachezaji wenzangu, na mashabiki wote kwa msaada wao mkubwa. Siwezi kusubiri kurejea uwanjani hivi karibuni.”

Wachezaji wenzake kama Marc Cucurella na Josh Acheampong, pamoja na Zach Abbott (aliyehusika kwenye mgongano huo), wamemtumia ujumbe wa kumtakia heri na kupona haraka.

Kabla ya tukio hilo la kusikitisha, Derry alikuwa mchezaji bora zaidi upande wa Chelsea. Uwezo wake wa kubadili uelekeo kwa kasi na kuwasumbua walinzi uliwafanya watazamaji kumlinganisha na staili ya uchezaji ya Jack Grealish.

Alionyesha ujasiri mkubwa, akihusika kwenye shambulizi la mapema lililomshirikisha Joao Pedro na Enzo Fernandez, pamoja na kujaribu kufunga kwa staili ya sarakasi dakika ya 25.

Derry amekuwa na msimu mzuri na timu ya Chelsea ya vijana (U21), akicheza michezo 29, kufunga mabao 12 na kutoa pasi za mabao nne. Kabla ya mechi ya jana, dakika zake pekee kikosini msimu huu zilikuwa kwenye michuano ya Kombe la FA dhidi ya Wrexham na Hull City.

Mashabiki wa “The Blues” kwa sasa wana matumaini ya kumuona tena uwanjani kabla ya msimu huu wa Ligi Kuu ya England haujafika tamati, huku afya yake ikiendelea kuimarika.