Home Habari za michezo SARE YA GONCALVES, KISASI NA KANUNI YA BARKER

SARE YA GONCALVES, KISASI NA KANUNI YA BARKER

0

DAKIKA 90 za mechi baina ya KMC dhidi ya Yanga itakayochezwa leo Jumatano saa 10:00 jioni kwenye Uwanja wa KMC Complex, Dar es Salaam, zinaweza kutumika kwa mambo mawili kama daraja la ubingwa.

Lakini, kocha wa Yanga, Pedo Goncalves ameahidi kasi ileile waliyoitumia katika mechi dhidi ya Simba (Muungano na Ligi Kuu) pamoja na ile ya Azm FC (Muungano).

Jambo la kwanza ni daraja la Yanga katika kuwania ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu kwani inakutana na timu dhaifu si tu ndani ya ligi hiyo msimu huu, bali zinapokutana timu hizo ambapo rekodi zinaonyesha katika mechi 15 za ligi, Yanga imeshinda 12, KMC ikipata ushindi mara moja, wakati sare ni mbili.

Kwa upande mwingine, inaweza kuwa daraja la kuishusha KMC ikipoteza mechi hiyo ama kuanza kujiinua kwa ushindi kwani inaburuza mkia na pointi tisa baada ya mechi 20, huku ikiwa haijapata ushindi ndani ya ligi katika mechi saba zilizopita zaidi ya kuambulia sare moja, sita ni vipigo.

KMC ambayo mara ya mwisho kushinda katika ligi ilikuwa Februari 3, 2026 ilipoichapa Mashujaa bao 1-0, tangu ilipoambulia sare mbele ya Yanga Aprili 10, 2021, haijapata matokeo mengine zaidi ya vipigo dhidi ya bingwa huyo mtetezi katika mechi tisa zilizofuatia huku pia ikiwa haina makali ya kucheka na nyavu, ikifunga mabao mawili, huku ikiruhusu 25.

Timu hizo zilipokutana duru la kwanza, Yanga iliibuka na ushindi wa mabao 4-1, hivyo leo itakuwa kazi kubwa kwa KMC kuizuia Yanga isipate ushindi mwingine huku ikiwa imetoka kuambulia sare ya 2-2 dhidi ya Simba.

Yanga ambayo sasa inaongoza ligi ikiwa na pointi 48, inapambana kusaka ushindi ili kuweka sawa hesabu zake kuelekea mwisho wa msimu ikihitaji kutetea ubingwa iliouchukua mara nne mfululizo, huku ikifahamu kwamba, nyuma yake kuna Simba inaikimbiza kwa tofauti ya pointi tano.

Akizungumzia mechi hiyo, Kocha Mkuu wa Yanga, Pedo Goncalves, amesema: “Tunarejea tena kwenye ratiba ngumu sana ya mechi mfululizo. Leo (jana) tunarejea kambini kuanza maandalizi yetu, jana (juzi) ilikuwa siku ya mapumziko kwa sababu tulikuwa kambini kwa wiki mbili mfululizo. Wakati mwingine tunahitaji kupumzika ili kupata nguvu na pia kutatua masuala yetu binafsi, na sasa kwa hakika tuna umakini kamili kwa ajili ya mchezo wa kesho (leo) dhidi ya KMC.

“KMC ni timu inayopambana kubaki kwenye Ligi Kuu, na tunawaheshimu sana wapinzani wetu wa kesho (leo). Kwetu sisi, tunapaswa kudumisha mtazamo ule ule, kuanzia kwa makocha hadi kwa wachezaji. Kucheza dhidi ya KMC kunapaswa kuwa na mtazamo sawa na ule tuliokuwa nao tulipocheza dhidi ya Azam na mara mbili dhidi ya Simba, katika mtazamo wangu, jambo hilo haliwezi kuwa tofauti.

“Hivyo basi, kwa ajili ya kesho (leo), tuna umakini wa hali ya juu tukijaribu kupata alama tatu muhimu dhidi ya timu yenye aina tofauti ya uchezaji. Tunapaswa kutafuta suluhu za kuwafunga na kuendelea kukabiliana na ratiba hii ngumu pamoja na ushindani mkali wa ligi.”

Kwa upande wa Kaimu Kocha Mkuu wa KMC, Iman Mwalupetelo, amesema: “Tumefanya kazi kwa ajili ya kuwaandaa wachezaji kisaikolojia kwa sababu ukiangalia nafasi ambayo tuko nayo sasa hivi, ni wa mwisho katika ligi, kwa wachezaji wengi wana presha lakini tunajaribu kuwajenga kisaikolojia kwamba ni mechi kama mechi zingine, cha msingi tufuate utaratibu jinsi plani ambayo tutaingia nayo tuitekeleze tu, hakuna lisilowezekana. “Kiujumla kwa ligi yote mechi zote ni ngumu japokuwa dhidi ya Yanga itakuwa ngumu kabisa kwa sababu aina ya timu ambayo tunakutana nayo ni kubwa katika nchi hii, yaani ina kila kitu.”

SIMBA VS JKT TANZANIA

Saa 12:15 jioni, Simba itaikaribisha JKT Tanzania kwenye Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar. Endapo ikishinda itaendelea kujiimarisha nafasi ya pili na kuifukuzia ya kwanza, lakini kama mambo yatakwenda sivyo, inaweza kujikuta ikishushwa na Azam kutegemea na matokeo yake ya jana ilipocheza dhidi ya Namungo.

Kama anavyoamini kocha wa Simba, Steve Barker kuwa bado wana nafasi ya kuwania ubingwa wa ligi msimu huu licha ya kupitwa na Yanga pointi tano, ili hilo liendelee kuwa na nguvu timu hiyo inapaswa kuifunga JKT Tanzania ambayo inashika nafasi ya nne na pointi 32.

“Matarajio ya kila mechi ni kuhakikisha tunashinda ili kujiweka nafasi nzuri ya kuwania ubingwa wa Ligi Kuu, mechi ni ngumu lakini wachezaji wapo tayari kwa kupambania malengo ya klabu,” amesema Barker.

Mechi ya mzunguko wa kwanza iliyopigwa Novemba 8, 2025, JKT Tanzania ikiwa mwenyeji ilifungwa mabao 2-1 na Simba, jambo ambalo kocha wa timu hiyo, Ahmad Ally amesema wanahitaji ushindi na siyo kupoteza kwa mara nyingine.

“Haitakuwa mechi rahisi, itakuwa ya mbinu zaidi. Mzunguko wa kwanza tulifungwa lakini matarajio yetu kwa sasa ni kuvuna pointi tatu,” amesema kocha Ally.

Simba inacheza na JKT ikiwa na pointi 43 ilizozipata katika mechi 20, imeshinda 12, sare saba imepoteza moja, inamiliki mabao 39, imeruhusu tisa. Wakati JKT Tanzania katika mechi 20 ilizocheza imeshinda nane sawa na sare, huku ikipoteza nne, inamiliki mabao 21, imeruhusu 20, ina pointi 32.

Rekodi zinaonyesha kwamba, mechi saba zilizopita Simba imeifunga JKT Tanzania mfululizo hali inayoonesha kuna kazi kubwa ya kufanywa na Wanajeshi hao.

Kwa ujumla, timu hizo zimekutana mara 11 ndani ya ligi, Simba ikishinda kumi, wakati JKT Tanzania nayo imeshinda moja, hakuna sare baina yao.

MTIBWA VS DODOMA

Mechi ya Mtibwa Sugar ambayo ni mwenyeji wa Dodoma Jiji itakayochezwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Dar kuanzia saa 2:30 usiku, Wakatamiuwa hao ndiyo wenye presha zaidi ya kupata matokeo ya ushindi ili kuondoka nafasi ya 11 waliyopo katika msimamo wa Ligi Kuu kabla ya mechi ya jana. Mtibwa imecheza mechi 20, imeshinda tano, sare nane, imepoteza saba, imefunga mabao 16, imeruhusu 24 na kukusanya pointi 23, huku Dodoma Jiji iliyocheza mechi 20, imeshinda sita, ina sare saba sawa na kupoteza, inamiliki mabao 18, imeruhusu 21, ina alama 25 katika nafasi ya nane kabla ya jana.

Nahodha wa Mtibwa, Oscar Masai, amesema: “Mechi itakuwa ngumu, tunahitaji ushindi ili kupanda nafasi za juu zaidi, hatutaki kurudi tulikotokea.”

Wakati kocha wa Dodoma Jiji, Aman Josiah akisema: “Ligi imefika pagumu, hakuna mechi nyepesi hasa kulingana nafasi tulizopo ambazo hakuna timu inaweza ikajihakikishia kusalia kwenye ligi, ni kama ushindani umebakia kwetu sisi wenyewe kwa wenyewe ukiondoa zile timu tatu za juu, pia haitakuwa mechi yenye mabao mengi hata ukicheza na timu iliyopo mkiani ngumu kupata mabao mengi, kikubwa ni kila kocha ana mbinu zake za kupata alama tatu na kuzuia usifungwe.”