Home Habari za michezo WAFUNGAJI BORA WA MABAO MUDA WOTE LIGI YA MAINGWA ULAYA

WAFUNGAJI BORA WA MABAO MUDA WOTE LIGI YA MAINGWA ULAYA

0

LONDON, ENGLAND: INAELEZWA kila mbabe ana mbabe wake. Lakini, kuna mazingira ambayo mbabe mmoja anaweza kuwa bila mbabe mwingine kujitokeza hadi anapomalizana na suala husika.

Ndivyo ilivyo hadi sasa huko Ulaya ambako Ligi ya Mabingwa imemshuhudia mbabe mmoja akitawala na kuacha rekodi ya ufungaji bora ikiendelea kusimama hadi sasa, licha ya kwamba ana misimu mitatu tangu alipoondoka huko, na kabla ya hapo akiwa na msimu mmoja nje ya michuano hiyo.

Hivyo, Cristiano Ronaldo tangu ashiriki mara ya mwisho michuano hiyo ni misimu minne sasa imepita.

CRISTIANO RONALDO (MABAO 140)

Cristiano Ronaldo ndiye mfungaji bora wa muda wote katika historia ya Ligi ya Mabingwa Ulaya akiwa na mabao 140 katika mechi 183 alizocheza.

Kwa sasa nyota huyo wa Ureno anacheza katika klabu ya Saudi Arabia ya Al Nassr, na kuna uwezekano mdogo wa kuongeza idadi hiyo ya mabao aliyoyakusanya akiwa Manchester United (21), Real Madrid (105) na Juventus (14).

Ronaldo pia anashikilia rekodi ya mabao mengi zaidi katika msimu mmoja wa Ligi ya Mabingwa Ulaya akiwa nayo 17 aliyofunga Real Madrid msimu wa 2013-14, ambapo waliibuka mabingwa baada ya kuifunga Atletico Madrid katika fainali.

Alifuata mafanikio hayo kwa kufunga mabao 16 msimu wa 2015-16.

Nyota huyo wa Ureno ameshinda tuzo ya mfungaji bora wa mashindano hayo mara saba, ambayo ni rekodi katika historia yote ya Kombe la Ulaya na Ligi ya Mabingwa Ulaya. Amefunga katika mechi 93 tofauti za ligi hiyo, sawa na asilimia 51 ya mechi alizocheza, huku mechi nane kati ya hizo akifunga hat-trick, rekodi anayoshirikiana na Lionel Messi.

Ronaldo amefunga dhidi ya wapinzani 38 tofauti katika historia yake ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, huku mabao yake 10 dhidi ya Juventus yakiwa mengi zaidi dhidi ya klabu moja katika historia ya mashindano hayo.

LIONEL MESSI (MABAO 129)

Lionel Messi ndiye mfungaji wa pili kwa mabao mengi katika historia ya Ligi ya Mabingwa Ulaya akiwa nayo 129. Hata hivyo, anashikilia rekodi ya kufunga mabao mengi zaidi kwa klabu moja katika historia ya michuano hiyo, kwani mabao 120 kati ya 129 alifunga akiwa Barcelona.

Aliongeza mabao mengine tisa baada ya kujiunga na mabingwa wa Ligue 1, Paris Saint-Germain, katika msimu wa kiangazi wa 2021, lakini kuna uwezekano mdogo sana wa kuongeza idadi hiyo baada ya kuhamia klabu ya Ligi Kuu Marekani (MLS), Inter Miami. Rekodi ya Messi ya kufunga dhidi ya wapinzani 40 tofauti katika Ligi ya Mabingwa Ulaya ni kubwa zaidi kuliko mchezaji yeyote, akimzidi Ronaldo mwenye 38. Mabao tisa ya Messi yalifungwa dhidi ya Arsenal (sawa na asilimia saba), ambayo ni timu aliyofunga zaidi dhidi yake katika ligi hiyo.

Kwa ujumla, mshindi huyo wa Kombe la Dunia 2022, Messi, amefunga katika misimu 18 tofauti ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, akifunga katika kila msimu tangu 2005-06 baada ya kukosa kufunga katika msimu wake wa kwanza wa 2004-05 alipocheza mechi moja tu Barcelona. Anashirikiana na Karim Benzema kwa rekodi ya kufunga katika misimu 18 ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, lakini Benzema alifunga katika kila moja ya misimu hiyo.

Messi pia anashirikiana na Ronaldo rekodi ya hat-trick nane, lakini yeye ndiye mchezaji pekee aliyewahi kufunga mabao matano katika mechi moja ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Alifanya hivyo katika ushindi wa Barcelona wa mabao 7-1 dhidi ya Bayer Leverkusen, Machi 2012, ikiwa sehemu ya msimu wake wa kihistoria wa 2011-12 ambapo alifunga mabao 73 katika mechi 60 za klabu.

ROBERT LEWANDOWSKI (MABAO 109)

Robert Lewandowski alifikia mabao 100 ya Ligi ya Mabingwa Ulaya Novemba 26, mwaka jana alipofunga kwa Barcelona dhidi ya klabu ya Ufaransa, Brest. Mabao 69 kati ya 109 alifunga akiwa Bayern Munich baada ya kuhamia kutoka Borussia Dortmund. Akiwa na mabao 23 Barcelona, anakuwa mchezaji wa pili katika historia ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kufunga mabao 10 au zaidi akiwa na klabu tatu tofauti baada ya Cristiano Ronaldo. Anashikilia rekodi ya Bayern Munich ya mabao mengi zaidi Ulaya, akimpita Gerd Muller (65). Pia anashikilia rekodi ya klabu hiyo ya mabao mengi zaidi katika msimu mmoja wa mashindano hayo alipofunga 15 msimu wa 2019-20 wakati Bayern walipotwaa ubingwa.

Kwa kufanya hivyo, alikuwa mchezaji wa kwanza kutoka Poland kumaliza msimu akiwa mfungaji bora wa mashindano ya klabu ya Ulaya. Mabao yake ya 108 na 109 alifunga dhidi ya Newcastle United katika hatua ya 16 bora msimu wa 2025-26, na hivyo kuvunja rekodi ya kufunga dhidi ya wapinzani wengi zaidi (41) katika historia ya mashindano hayo.

KARIM BENZEMA (MABAO 90)

Baada ya kuhamia Al-Ittihad ya Saudi Arabia, Juni 2023, Karim Benzema anaonekana kuwa na uwezekano mdogo sana wa kuongeza mabao yake 90 ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Benzema amefunga katika misimu mingi zaidi ya ligi hiyo bila kukosa kufunga, akiwa amefunga katika misimu yote 18 aliyoshiriki tangu alipoanza 2005-06 akiwa Lyon ya Ufaransa.

Alishinda tuzo ya mfungaji bora wa Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa mara ya kwanza msimu wa 2021-22, akiwa na mabao 15 yaliyoisaidia Real Madrid kutwaa ubingwa, ingawa hakufunga katika fainali dhidi ya Liverpool jijini Paris. Mabao yake 78 akiwa Real Madrid yanamuweka nyuma ya Cristiano Ronaldo pekee (105) katika historia ya klabu hiyo.

RAUL GONZALEZ (MABAO 71)

Mchezaji wa zamani wa timu ya taifa ya Hispania, Raul Gonzalez ni mfungaji wa tatu kwa mabao mengi Real Madrid katika Ligi ya Mabingwa Ulaya (66), huku jumla yake ya mabao 71 ikiwa ya tano kwa wachezaji wote katika historia ya mashindano hayo. Raul alikuwa mfungaji bora wa mashindano hayo hadi Novemba 2014 alipopitwa na Messi na Ronaldo. Pia alikuwa mchezaji wa kwanza kufikia mabao 50 katika historia ya mashindano hayo alipofanya hivyo Septemba 2005.

Ndiye aliyekuwa mchezaji wa kwanza wa Real Madrid kufikisha mabao 50 Ulaya baada ya Alfredo Di Stefano kufunga mabao 49 kwa klabu hiyo katika mashindano ya Ulaya.

Msimu wake wa mwisho wa Ligi ya Mabingwa Ulaya ulikuwa akiwa Schalke 04 nchini Ujerumani 2010-11, ambapo alifunga mabao matano akiwa na umri wa miaka 33, na kufikisha jumla ya mabao 71.  Hii ni zaidi ya mara mbili ya mchezaji mwingine yeyote wa Hispania katika historia ya mashindano hayo, ambapo Fernando Morientes ndiye anayemkaribia zaidi akiwa na mabao 33.

MASTAA WENYE MABAO 50+

KYLIAN MBAPPE (MABAO 70)

Kylian Mbappe alifikia mabao 50 ya Ligi ya Mabingwa Ulaya katika mechi ya Real Madrid dhidi ya Atalanta, Desemba 10, 2024, ambapo akiwa na umri wa miaka 25 na siku 356 alikuwa mchezaji wa pili mwenye umri mdogo kufikia hatua hiyo baada ya Messi ambaye alifikia mabao 50 akiwa na miaka 24 na siku 284 alipofunga dhidi ya AC Milan, Aprili 2012.

Kwa kufikia mabao 50 katika mechi 79, Mbappe alikuwa mchezaji wa nne kwa kasi zaidi kufikia mabao 50 nyuma ya Ruud van Nistelrooy (mechi 62), Messi (66) na Lewandowski (77), ingawa Harry Kane pia baadaye alimzidi. Mbappe alifunga mabao 15 katika msimu wa 2025-26. Ni Cristiano Ronaldo pekee aliyewahi kufunga zaidi ya hayo katika msimu mmoja wa mashindano hayo.

THOMAS MULLER, ERLING HAALAND (MABAO 57)

Tangu alipoanza kucheza mashindano hayo 2008-09, Thomas Müller alifunga mabao 57 na kutoa pasi za mabao 25. Ameshinda ubingwa  mara mbili akiwa Bayern Munich msimu wa 2012-13 na 2019-20.

Kwa upande wake Erling Haaland aliweka historia Septemba 2025 alipofunga bao lake la 50 akifanya hivyo kwa kasi zaidi kuliko mchezaji yeyote katika historia ya mashindano hayo aliyo nayo hadi sasa. Alifunga mabao akiwa Salzburg, Borussia Dortmund na Manchester City na kufikia mabao 50 katika mechi 49 pekee, akivunja rekodi ya Ruud van Nistelrooy ya mechi 62. Alifunga mabao mawili zaidi katika mchezo wa pili wa msimu wa 2025-26 dhidi ya Monaco, na kufikisha mabao 52 katika mechi 50 za kwanza rekodi kubwa zaidi kuliko Van Nistelrooy aliyekuwa na 43.

RUUD VAN NOSTELROOY (MABAO 56)

Ruud van Nistelrooy alifunga mabao 56, ingawa angeweza kuwa na zaidi kama angecheza mechi nyingi mapema katika maisha yake ya soka, kwani alikuwa na mechi 11 pekee akiwa PSV kabla ya kufikisha miaka 25 na kujiunga na Manchester United katika Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Aliweka rekodi ya kufikisha mabao 50 kwa kasi kubwa kabla ya Haaland na wengine, akifanya hivyo katika mechi 62, lakini alifikia hatua hiyo akiwa na umri wa miaka 31. Amefunga mabao 35 kwa Manchester United, ambayo ni rekodi ya klabu hiyo katika Ligi ya Mabingwa mbele ya Wayne Rooney (30) na Ryan Giggs (28).

HARRY KANE (MABAO 52)

Harry Kane alifunga mabao yake ya 49 na 50 ya Ligi ya Mabingwa Ulaya katika ushindi wa Bayern Munich dhidi ya Atalanta, Machi 2026.

Alifikia mabao 50 katika mechi 66, ikiwa ni haraka zaidi kuliko wengi, nyuma ya Haaland (49 mechi) na Van Nistelrooy (62 mechi). Idadi ya mechi 66 ni sawa na ile ya Messi alipofikia mabao 50.

THIERRY HENRY (MABAO 50)

Thierry Henry alifunga mabao 50 katika Ligi ya Mabingwa akiwa na klabu tatu, Arsenal (35), Barcelona (8) na Monaco (7). Alianza vizuri akiwa Monaco akifunga mabao sita katika mechi tano za kwanza akiwa na umri wa miaka 20 kabla ya kuhamia Arsenal msimu wa 1999-2000.  Mabao yake 35 kwa Arsenal yanamfanya kuwa mfungaji bora wa klabu hiyo katika historia ya mashindano hayo.

MOHAMED SALAH (MABAO 50)

Mohamed Salah alifikia mabao 50 ya Ligi ya Mabingwa Ulaya katika ushindi wa Liverpool dhidi ya Galatasaray, Machi 2026.

Kwa bao hilo, alikuwa mchezaji wa kwanza kutoka Afrika kufikia alama hiyo katika historia ya mashindano hayo.