Home Habari za michezo PSG 5-4 BAYERN NGOMA HII KURUDIWA LEO

PSG 5-4 BAYERN NGOMA HII KURUDIWA LEO

0

MUNICH, UJERUMANI: Mengi yameshasemwa kuhusu faida na hasara za mfumo uliopanuliwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya, lakini jambo moja halijawahi kujadiliwa; uwezo wa hatua za mtoano kutoa burudani. Na Jumanne, wiki iliyopita katika Uwanja wa Parc des Princes, Paris, Ufaransa wababe walitoa  burudani isiyo na kifani. Je watarudia tena kesho?

PSG waliifumua Bayern Munich kwa mabao 5-4 katika mechi ya kwanza ya nusu fainali kwenye moja ya mechi za kusisimua zaidi kuwahi kushuhudiwa katika mashindano hayo.

Kwa mabao tisa, huo ulikuwa ni mchezo wa nusu fainali uliokuwa na mabao mengi zaidi katika historia ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.

NGUVU YA KIPEKEE NA USHAMBULIAJI

Kwa kuzingatia vipaji vilivyokuwepo uwanjani mabao tisa hayakupaswa kushangaza sana.

Katika mashindano yote, Bayern Munich ina uwiano wa mabao 3.4 kwa mchezo msimu huu na wamekuwa wakifunga mara nyingi zaidi kuliko timu nyingine yoyote katika ligi tano bora za Ulaya, huku PSG ikiwa na uwiano wa mabao 2.4 ikiwa ya tatu.

Kwa PSG kuwa na mabao mengi zaidi Ulaya 43 na Bayern 42, pia ni msimu wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa kuwa na timu mbili zilizofikisha mabao 40 au zaidi. Je, hilo linashangaza kwa kuzingatia washambuliaji waliokuwepo?

Wachezaji wanne walioanza mchezo – Harry Kane, Michael Olise, Ousmane Dembele na Khvicha Kvaratskhelia – wako ndani ya wachezaji saba wanaopigiwa upatu zaidi kuwania Ballon d’Or. Dembele, bila shaka ndiye mshindi wa sasa.

Na hiyo ni kabla ya kumtaja Luis Diaz aliyefunga bao lake la 26 Jumanne hiyo baada ya udhibiti wa ajabu wa mpira kwa mguu wa kwanza. Ukiwajumlisha Kane (54) na Olise (20), safu ya ushambuliaji ya Bayern imechangia mabao 100 kwa pamoja katika mashindano yote msimu huu.

Hii ni mara ya tano tangu msimu wa 2013-14 kwa safu ya ushambuliaji kufikisha mabao 100 kwa pamoja, na safu ya Bayern ni ya tatu kufanya hivyo.

Lionel Messi, Luis Suarez na Neymar Jr walifanya hivyo kwa misimu mitatu mfululizo kuanzia 2014-15 hadi 2016-17, huku Cristiano Ronaldo, Karim Benzema na Gareth Bale/James Rodríguez (wote 17) wakifanya hivyo msimu wa 2014-15.

UMALIZIAJI WA KIPEKEE

Sasa siyo kwa kuharibu sherehe, lakini mabao tisa yalitokana na safu bora za ushambuliaji. Kwa maneno mengine mabao manne zaidi kuliko ambavyo labda yangetokea kulingana na ubora wa nafasi. Tofauti hiyo ilichangiwa zaidi na PSG waliofunga mara tano.

Hiyo ilikuwa mara ya kwanza katika rekodi tangu 2003-04 kwa timu kuwa na mashuti matano au zaidi yaliyoenda langoni na kufunga yote katika mchezo wa hatua ya mtoano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Lakini hilo ndilo linaloweza kutokea wakati safu za ushambuliaji zilizojaa nyota kutoka pande zote mbili zikiwa katika kiwango cha juu.

Mchezo ulichezwa kwa kasi ya umeme na hakuna wakati ambao tempo ilipungua. Pande zote mbili zilionekana kuwa na nguvu, fiti na zenye hamasa na zilichanganya ubora wa kiufundi na nguvu ya kimwili.

Bayern tayari wametwaa ubingwa wa Bundesliga. PSG bado hawajathibitisha  ubingwa wa Ligue 1, lakini wako juu katika msimamo.

Klabu zote mbili zilifanya mzunguko wa wachezaji kwa urahisi kwenye ligi zao za nyumbani ambako huwa ndizo zenye mvuto pia.

Mchezo ulikuwa wa kasi na wa kuvutia na hakukuwa na upande uliokuwa na wasiwasi wa kujibaoa nyuma na mastaa wote walikuwa na nia ya kushambulia. Ilionekana kama mpira ulikuwa hauishi uwanjani, mchezo ukifanana na mpira wa kikapu wenye mashambulizi ya mfululizo.

MPIRA UWANJANI

Kwa muda wa mpira kuwa uwanjani ilikuwa asilimia 54.9 ya mchezo, chini kidogo ya wastani wa Ligi ya Mabingwa msimu huu (58.3%).

Lakini hilo linaweza kuelezwa zaidi na idadi kubwa ya mabao. Zaidi ya dakika 10 zilipotea kutokana na sherehe za mabao na ucheleweshaji wa kuanza upya mchezo.

Tukitazama maeneo ya mchezo ambayo wachezaji wanaweza kudhibiti moja kwa moja, mojawapo ilionekana wazi kwamba mipira ya kurusha (throw-ins).

PSG na Bayern walichukua sekunde 13.7 kuanza tena mchezo baada ya kurusha, haraka kuliko timu yoyote ya Ligi Kuu England msimu huu (Manchester City ndio wana haraka zaidi kwa sekunde 14.9).

Katika dunia (hasa Ligi Kuu England) ambako ulimwengu unazidi kuona timu zikichelewa kurusha mipira mirefu ndani ya eneo la hatari, ilikuwa faraja kuona timu mbili zikiwa na haraka ya kurudisha mpira uwanjani.

Mapema mwezi huu, rais wa Napoli, Aurelio De Laurentiis, alipendekeza mabadiliko makubwa yenye lengo la kuboresha soka ili kuvutia kizazi kipya na bilionea huyo mwenye umri wa miaka 76 alisema mfumo wa sasa wa dakika 90 ni mrefu sana kwa kizazi kilichokulia kwenye michezo ya video, akipendekeza kupunguzwa kwa muda wa vipindi na kuondolewa kwa kadi za njano na nyekundu.