YANGA imeendelea kuchachamaa katika mbio za kuwania ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kuibuka na ushindi muhimu wa bao 1-0 dhidi ya KMC FC, katika mchezo uliochezwa Uwanja wa KMC Complex, Mwenge.
Ushindi huo ulipatikana kupitia kwa kiungo mshambuliaji Allan Okello aliyefunga bao pekee la mchezo dakika ya 65, akimalizia kwa ustadi pasi safi kutoka kwa Shekhan Ibrahim, bao lililowapa furaha mashabiki wa Wananchi.
Katika dakika 45 za kwanza, timu zote zilionekana kucheza kwa tahadhari huku kila upande ukijaribu kutengeneza nafasi za kufunga, lakini uimara wa safu za ulinzi ulifanya kipindi hicho kumalizika bila ya bao licha ya presha kubwa iliyokuwepo uwanjani.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi zaidi kwa Yanga waliokuwa na dhamira ya kutafuta ushindi, jambo lililowalipa baada ya Okello kufungua ukurasa wa mabao na kuifanya KMC kuanza kucheza kwa presha wakitafuta kusawazisha bila mafanikio.
Matokeo hayo yanaendelea kuipa Yanga nguvu katika mbio za kutetea ubingwa wao, huku wakizidi kujijengea pengo la alama dhidi ya wapinzani wao wakubwa Simba, katika vita vinavyozidi kupamba moto kadri ligi inavyoelekea ukingoni.