Ratiba yao pia haionekani kuwa rafiki. Bado wanakutana na vigogo wawili wa ligi, Azam na Simba huku pia wakiwa na mechi ngumu dhidi ya TRA United na Mashujaa.
Mechi zinazoweza kubeba matumaini yao ni zile dhidi ya Fountain Gate, Mtibwa Sugar, Coastal Union na Namungo ambazo zote zinapambana kwenye ukanda wa chini.
Kitu kingine kinachowaumiza KMC ni safu yao ya ushambuliaji. Wamefunga mabao manane pekee katika mechi 21, idadi ndogo zaidi ligi nzima. Takwimu hiyo inaonyesha kwanini wamekuwa wakipata shida kubadili sare au vipigo kuwa ushindi.
Ukuta wao bado haujawa imara baada ya kuruhusu mabao 32, wastani wa zaidi ya bao moja kwa kila mchezo. Katika hatua kama hii ya msimu, tofauti ndogo tu kwenye safu ya ulinzi inaweza kuamua hatima ya timu.
Kwa sasa, picha halisi inaonyesha KMC haina nafasi ya kufanya makosa mengi tena. Kila kipigo kinaisogeza karibu zaidi kwenda Ligi ya Championship na kama haitabadilika, huenda ikawa timu ya kwanza kushuka daraja kabla msimu haujafika mwisho.
Mechi za KMC zilizobaki ni dhidi ya Fountain Gate (Mei 10, nyumhani), Mtibwa Sugar (Mei 14, ugenini), Pamba Jiji (Mei 20, nyumbani), Azam (Mei 25, ugenini), TRA United (Juni 12, nyumbani), Coastal Union (Juni 15, ugenini), Namungo (Juni 24, nyumbani), Mashujaa (Juni 27, ugenini) na Simba (Juni 30, ugenini).
Wakati huohuo, KMC ambayo imetoka kuchapwa bao 1-0 na Yanga, kuna kitu beki wa kikosi hicho, Mudathir Nassor kuhusu washambuliaji wa mabingwa hao watetezi.
Nassor amesema pamoja na KMC kupoteza nyumbani kwa bao 1-0 dhidi ya Yanga, lakini hakukuwa na ugumu mkubwa kuwazuia washambuliaji wa wapinzani hao kutokana na aina yao ya uchezaji kufanana.
Akizungumza na Mwanaspoti, Mudathir amesema aliweza kuwasoma vizuri washambuliaji wa Yanga, Prince Dube na Laurindo Aurelio ‘Depu’ jambo lililomsaidia kutowapa nafasi ya kufanya madhara makubwa langoni mwa KMC.
“Hakuna ugumu wa kuwakaba washambuliaji wa Yanga kwa sababu aina yao ya uchezaji inafanana ndio maana niliweza kuwasoma vizuri na kutowapa uhuru,” amesema Mudathir.
Beki huyo alieleza kuwa, changamoto kubwa kwa upande wa KMC haikuwa kufika langoni mwa wapinzani, bali kushindwa kutumia nafasi walizozitengeneza kwenye eneo la ushambuliaji.
“Ubora wetu ulikuwa kwenye kutengeneza nafasi na sio kwamba tulikuwa hatufiki langoni kwa Yanga, tulikuwa tunafika ila hatukuwa na ubora kwenye eneo la mbele,” amesema.
Mudathir alieleza kuwa, hakuna mchezaji anayefurahia kufungwa, huku akibainisha kwamba KMC itaendelea kupambana kuhakikisha inabaki salama kwenye ligi.
“Matokeo yanatuumiza, hakuna anayependa kufungwa. Tutaendelea kupambana, tukishuka haya, tukisalia basi itakuwa jambo la kheri, lakini kikubwa kwa sasa tunapambana,” amesema.
Aidha, beki huyo amesema michezo mikubwa ya aina hiyo inaendelea kumpa uzoefu kutokana na kuwa huu ni msimu wake wa kwanza ndani ya KMC tangu alipojiunga na timu hiyo katika dirisha dogo Januari 2026 akitokea Zimamoto ya Zanzibar.