Villa ilifanikiwa kusawazisha jumla ya mabao dakika saba kabla ya mapumziko, pale Watkins alipomalizia krosi ya Buendia kutoka upande wa kushoto.
Dakika 13 baada ya kipindi cha pili kuanza, Villa iliongeza bao la pili baada ya mwamuzi Glenn Nyberg kutoa penalti kufuatia mapitio ya VAR, ambapo Nikola Milenkovic alionekana kumvuta Pau Torres.
Watkins pia alifunga bao ambalo baadaye lilikataliwa kwa kuotea, huku kipa Emiliano Martínez akiokoa hatari ya Chris Wood upande wa Forest, kabla ya McGinn kufunga mabao mawili ya haraka yaliyohitimisha ushindi huo mkubwa.
FREIBURG 3-1 BRAGA
Ushindi wa jumla wa mabao 4-3, umeifanya SC Freiburg kufuzu fainali yao ya kwanza kabisa ya michuano ya Ulaya baada ya kuifunga SC Braga waliobaki na wachezaji 10 katika mchezo wa marudiano wa nusu fainali ya Europa League uliochezwa Alhamisi, Mei 7, 2026.
Ikiwa mbele kwa jumla ya mabao 2-1 kutoka mchezo wa kwanza, Braga ilipata pigo kubwa baada ya Mario Dorgeles aliyefunga bao la ushindi la dakika za mwisho nchini Ureno kuonyeshwa kadi nyekundu ya moja kwa moja kwa kumchezea faulo ya makusudi Jan-Niklas Beste.
Freiburg haikuchukua muda kutumia faida hiyo ya idadi ya wachezaji, wakitangulia kuongoza kupitia tukio lililoanzia kwa Jean-Baptiste Gorby kushindwa kuokoa mpira vizuri, uliogonga goti la Lukas Kubler kabla ya kuingia wavuni ukigusa mwamba wa mbali.
Ingawa bao la kwanza lilikuwa na bahati kidogo, hapakuwa na bahati yoyote kwenye bao la pili la kuvutia la Yohan Manzambi dakika nne kabla ya mapumziko.
Kiungo huyo mwenye umri wa miaka 20, alijitengenezea nafasi nje ya eneo la penalti na kupiga shuti kali la mguu wa kulia lililojaa wavuni kona ya mbali, jambo lililosababisha shangwe kubwa kwa mashabiki wa Freiburg ndani ya Uwanja wa Europa-Park Stadion.
Victor Gomez aliugonga mwamba baada ya kumpita kipa wa Freiburg Noah Atubolu mwishoni mwa kipindi cha kwanza, huku Vincenzo Grifo naye akizuiwa na mwamba huo kwa shuti la chini mapema kipindi cha pili.
Kipa wa Braga Lukas Hornicek aliokoa hatari mbili za kushangaza dhidi ya Igor Matanovic na Matthias Ginter dakika 20 kabla ya mwisho, lakini hakuwa na la kufanya wakati Kubler alipoongeza bao la tatu kwa kichwa kikali.
Bao la kichwa la karibu la Pau Victor liliwapa Braga matumaini dakika saba baadaye, lakini timu hiyo ya kocha Carlos Vicens haikuweza kurejea mchezoni.
Kocha Julian Schuster ushindi wake huo ulikuwa wa 11 mfululizo kwa Freiburg nyumbani katika Europa League, ikisawazisha rekodi ya muda wote iliyowekwa na Sevilla FC kati ya Aprili 2014 na Machi 2016.