Argentina Yazindua Sanamu La Messi
NEUQUEN, ARGENTINA: ARGENTINA imezindua sanamu ya Messi yenye uzito wa tani 70, ikiwa ni kubwa zaidi duniani ambayo inalenga kuvutia watalii katika Jiji la Cutral Co lililopo mkoani Neuquen ambalo linaaminika kuwa ndilo kubwa zaidi duniani kuwahi kujengwa kwa heshima ya nyota huyo wa soka.
Sanamu hilo limebuniwa na msanii wa eneo hilo, Aldo Beroisa, likimuonyesha Messi akiwa amevaa jezi ya timu ya taifa ya Argentina huku akiwa ameshika Kombe la Dunia walilolinyakua nchini Qatar 2022.
Muundo huo umejengwa kwa fremu ya chuma na kufunikwa kwa kiasi kikubwa na saruji, ukiwa na uzito unaokadiriwa kufikia tani 70. Kwa ukubwa huo, umeweka rekodi mpya kama sanamu kubwa zaidi kuwahi kujengwa kwa heshima ya mshindi huyo wa Ballon d’Or.
Mamlaka za Cutral Co zinaamini kuwa sanamu hilo litachochea utalii katika Mkoa wa Neuquen kwa kuvutia mashabiki wa Messi na soka la Argentina kutoka sehemu mbalimbali duniani, huku likiongeza hadhi ya mji huo ambao tayari unafahamika kama “mji mkuu wa sanamu”.
Uzinduzi wa sanamu la Messi umefanyika wakati akiendelea kuiongoza Argentina katika Kombe la Dunia 2026, ambako nyota huyo mwenye umri wa miaka 39 alianza kwa kiwango cha juu akifunga hat-trick katika ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Algeria kabla ya kufunga mabao mawili katika ushindi wa 2-0 dhidi ya Austria. Kwa mabao hayo, Messi ameweka rekodi mpya ya kuwa mfungaji bora wa muda wote.