Maumivu Ya Dakika Ya 86 Timu Tatu Afrika
ATLANTA, MAREKANI: KATIKA matukio yaliyotikisa mashabiki wa soka duniani, timu tatu za Afrika zimeondolewa kwa maumivu makubwa katika hatua ya 32 bora ya Kombe la Dunia 2026 baada ya kuruhusu mabao ya ushindi katika dakika ya 86.
Ivory Coast 1–2 Norway
Katika mchezo uliochezwa jijini Houston, Marekani, Ivory Coast walikabiliana na Norway katika mechi iliyokuwa na ushindani mkali kuanzia dakika ya kwanza. Ivory Coast walisawazisha dakika ya 74 kupitia kwa mshambuliaji Amad Diallo, akimalizia pasi murua kutoka kwa Nicolas Pepe.
Mapema, Norway ilifunga bao la dakika ya 39 kupitia winga Antonio Nusa aliyepokea asisti ya Erling Haaland. Hata hivyo, dakika ya 86, mshambuliaji hatari, Haaland, alipokea krosi ya chini kutoka upande wa kulia kwa beki wa kati Patrick Berg na kuipatia Norway bao la pili na la ushindi lililohitimisha safari ya Ivory Coast katika mashindano hayo.
DR Congo 1–2 England
Katika mechi nyingine iliyochezwa Miami, DR Congo ilipambana dhidi ya England ikafanikiwa kutangulia kupitia bao la dakika ya saba lililofungwa na winga Brian Cipenga, baada ya shambulizi la kushtukiza (counter attack) akipokea pasi kutoka kwa Chancel Mbemba.
Mechi ilipoonekana kuelekea muda wa nyongeza, mashabiki wa DR Congo walikuwa tayari kusherehekea angalau sare. Lakini dakika ya 86, Harry Kane alifunga baada ya kuwazungusha mabeki wa DR Congo na kuipiga shuti kali akiwa amebanwa lililotinga nyavuni na kuwa 2–1. Bao hilo liliwatoa DR Congo kwenye mashindano, licha ya awali kuukamata mchezo ipasavyo.
Senegal 2–3 Ubelgiji
Katika mchezo wa kusisimua zaidi, Senegal walipambana na Ubelgiji katika mechi iliyokuwa na mabao mengi na mabadiliko ya kasi.
Senegal walitangulia dakika ya 24 kupitia Habib Diarra aliyefunga kwa shuti kali akipokea asisti kutoka kwa Sadio Mane, kisha walipata bao la pili kupitia kwa Ismaila Sarr aliyepokea pasi ndefu kutoka kwa Moussa Niakhate katika dakika ya 51.
Ukisikia maumivu kwa Senegal na Afrika, basi hayo ndo yaliyokuwa maumivu kwani iliongoza kwa mabao 2-0 hadi dakikia ya 86 kabla ya mtokea benchi Romelu Lukaku kutupia bao la kwanza akipokea pasi kutoka kwa Thomas Meunier kabla ya Leandro Trossard kutoa asisti kwa Youri Tielemans aliyesawazisha katika dakika ya 89 kisha Tielemans kutupia bao la tatu kutokana na penalti iliyotokana na kufanyiwa madhambi ndani ya eneo la hatari. Hadi mwisho ilikuwa Senegal 2-3 Ubelgiji.
Kwa ujumla katika mecho zote tatu takwimu zinazoonyesha kuwa Ivory Coast walimiliki mpira kwa asilimia 48, DR Congo 46 dhidi ya England, na Senegal walikuwa na asilimia 52 ya umiliki dhidi ya Ubelgiji.
Hata hivyo, tofauti kubwa ilionekana kwenye ufanisi wa mashambulizi ya mwisho, ambapo timu za Ulaya zilikuwa na umakini mkubwa zaidi katika dakika za mwisho.
Kwa pamoja, timu hizo tatu za Afrika zilipiga jumla ya mashuti 27 yaliyolenga lango, lakini zilifunga mabao 4 pekee, wakati wapinzani wao walitumia nafasi chache zaidi lakini kwa ufanisi mkubwa.
Kuondolewa kwa Ivory Coast, DR Congo na Senegal kunatoa somo kuhusu umuhimu wa umakini hadi kipenga cha mwisho. Katika soka la kiwango cha Kombe la Dunia, dakika moja inaweza kubadilisha historia ya miaka mingi ya maandalizi.