Simba SC

Ni Nafasi Nyingine Kwa Jonathan Sowah

Vardo July 16, 2026 10:57 pm

JONATHAN Sowah kwa taarifa tulizonazo hapa kijiweni ni kwamba anarudi nchini kujiunga na Singida Black Stars.

Inaonekana tayari mkataba wake na Simba umeshavunjika kwa kifo cha kawaida baada ya kutokea utofauti baina yao.

Kwanza kijiwe kinakiri wazi kwamba Jonathan Sowah ni miongoni mwa washambuliaji wazuri ambao wamebahatika kucheza katika Ligi yetu siku za hivi karibuni.

Anajua kufunga na ni aina fulani ya mshambuliaji ambaye anapokuwepo uwanjani, mabeki na makipa wa timu pinzani huwa wanapoteza amani na utulivu wao.

Changamoto kubwa ambayo inaonekana kumuumiza Sowah ni ya nje ya uwanja jambo linalomfanya asiwe anadumu katika timu mbalimbali ambazo amekuwa anazichezea.

Sasa kama anarudi Singida Black Stars, bila shaka ni fursa muhimu kwa Sowah kujibu kwa vitendo yale mambo hasi ambayo yamekuwa yakizungumzwa dhidi yake.

Kile ambacho anajulikana anaweza kukifanya, anatakiwa akifanye kwa kiwango na ubora wa hali ya juu zaidi na kile kinachoaminika ni udhaifu wake basi anapaswa kukirekebisha ili kisimuathiri.

Ni fursa nyingine kwa Sowah kusafisha jina lake hapa nchini baada ya taswira isiyovutia ambayo baadhi wamemjengea kuanzia alipokuwa akiitumikia Singida Black Stars hadi alipotua Simba na sasa amerudi Singida.

Vodacom Yadhamini Mashindano Ya Golf Ya Corporate Masters 2026 Trossard Aiteka Istanbul, Mashabiki Wapagawa Kumshuhudia