Sio Mpira Tena! Biashara Mpya ya Pogba Saudi Arabia Baada ya Kutemwa Monaco
RIYADH, SAUDI ARABIA – Baada ya kuachana na klabu ya Monaco ya Ufaransa kutokana na changamoto za majeraha ya muda mrefu, aliyekuwa kiungo wa kimataifa wa Ufaransa, Paul Pogba, ameelekeza nguvu zake kwenye uwekezaji mpya wa mamilioni ya dola.
Nyota huyo, anayekadiriwa kuwa na utajiri wa takribani Dola 125 milioni kutokana na mikataba minono akiwa Manchester United, Juventus na udhamini wa kampuni kama Adidas, sasa ameingia kwa kishindo kwenye mchezo wa mbio za ngamia nchini Saudi Arabia.
Uwekezaji Kwenye Mbio za Ngamia (Al Haboob) Pogba amekuwa mwanahisa na mwekezaji kwenye klabu ya mbio za ngamia inayofahamika kama Al Haboob, iliyoanzishwa na wafanyabiashara wa Saudi Arabia, Omar Almaeena na Safwan Modir. Mchezaji huyo anapanga kununua ngamia mwenye thamani ya Dola 5 milioni kwa ajili ya kuimarisha timu yake.
“Ushiriki wa Paul unalenga kuunganisha mchezo huu na umaarufu wa kimataifa. Yupo kama mwekezaji na mwanahisa anayeelewa thamani ya kukuza mchezo huu duniani,” alisema Almaeena.
Biashara ya Mamilioni ya Dola Mbio za ngamia katika nchi za Ghuba (GCC) kama Saudi Arabia, UAE, Qatar na Oman zimekuwa biashara kubwa na ya kifahari inayovutia zawadi za zaidi ya Pauni 4 milioni kwenye mashindano mbalimbali.
Wamiliki wa klabu hiyo wanapanga kupanua mchezo huo hadi barani Ulaya ndani ya miezi 14 ijayo, huku pia wakiwa kwenye mazungumzo ya kumvuta legendari wa mpira wa kikapu (NBA), Shaquille O’Neal, kujiunga kama mwekezaji mwingine.