Home Simba SC GOMEZ: TUNATAKA KUSHINDANA NA MAZEMBE, AL AHLY AFRIKA

GOMEZ: TUNATAKA KUSHINDANA NA MAZEMBE, AL AHLY AFRIKA


KOCHA mkuu wa klabu ya Simba, Didier Gomes Da Rosa amefunguka kuwa malengo yake ni kuhakikisha anatengeneza kikosi imara ambacho kitakuwa na uwezo wa kushindana dhidi ya timu kubwa barani Afrika kama TP Mazembe na Al Ahly.

Gomez alitangazwa rasmi kuwa kocha mkuu wa klabu ya Simba Jumapili ya Januari 24 akichukua nafasi iliyoachwa na Mbelgiji, Sven Vandenbroeck ambaye alijiuzulu nafasi hiyo Januari 7, mwaka huu muda mfupi tu baada ya kuifikisha Simba kwenye hatua ya Robo fainali ya michuano ya Ligi ya mabingwa Afrika.

Gomez tayari amesimamia mazoezi ya kikosi chake kwa siku tatu mfululizo katika maandalizi ya michuano ya Simba Super Cup iliyoanza jana na kushirikisha timu tatu ambazo ni Al Hilal, TP Mazembe na mwenyeji Simba.

Akiwa katika mazoezi hayo Da Rosa alionekana kukazia zaidi katika ufundishaji wa pasi fupifupi na mazoezi magumu.

Akizungumzia mipango yake, Gomez alisema: “Nafurahi kuwepo hapa, nimejifunza vitu vingi ndani ya muda mfupi, vijana wangu wanaonekana kuwa na ari kubwa na wanajituma sana mazoezini.

“Malengo yetu ni kufanya vizuri kwenye kila michuano tunayoshiriki, lakini tunaendelea kuwekeza nguvu kubwa katika kuhakikisha tunakuwa na kikosi imara ambacho kitaweza kushindana dhidi ya timu kubwa kama TP Mazembe na Al Ahly kwenye michuano ya Afrika.

“Simba ni miongoni mwa klabu 16 bora barani Afrika na inaheshimika sana mbele ya wapinzani wake hivyo nasi ni lazima tuhakikishe tunakuwa kweli washindani wa kweli dhidi ya wapinzani wetu,”

SOMA NA HII  SIMBA YAWAITA MASHABIKI KUELEKEA SIMBA DAY