Home Simba SC SIMBA YATOA TAMKO KUHUSU HATMA YA MORRISON

SIMBA YATOA TAMKO KUHUSU HATMA YA MORRISON


 UONGOZI wa Simba umesema kuwa wale waliokuwa wanafikiria nyota wao Bernard Morrison anaumwa na atakaa nje ya uwanja kwa muda wa miezi sita wasahau jambo hilo kwa kuwa raia huyo wa Ghana yupo fiti.

Baada ya fainali ya Kombe la Mapinduzi, Januari 13 visiwani Zanzibar ilielezwa kuwa nyota huyo anaumwa hernia na hatakuwa ndani ya uwanja kwa muda wa miezi sita.

Morrison alishuhudia fainali ya Kombe la Mapinduzi kati ya Yanga ambao ni mabosi wake wa zamani dhidi ya Simba akiwa benchi na licha ya kufanya mazoezi aliishia kutazama akiwa amekaa kwenye benchi la ufundi na Kaimu Kocha, Seleman Matola.

Kwenye mchezo huo ndani ya dakika 90 zilikamilika kwa timu zote kutoshana nguvu na mshindi alipatikana kwa mikwaju ya penalti ambaye ni Yanga kwa ushindi wa penalti 4-3.

Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara amesema:”Wale ambao wanafikiria Morrison hatacheza na atakuwa nje ya uwanja kwa muda wa miezi sita wasahau hadithi hizo kwani mwamba yupo sawa na atacheza kwenye Simba Super Cup mwanzo mwisho.

“Unajua nilikuwa ninaskia kwamba wanadai mwamba ana hernia sijui ana nini nilikuwa ninaangalia tu maana nikimuona mwamba naona yupo sawa na anaendelea na mazoezi hivyo wale waliokuwa wanamuombea mabaya wasahau mzee atakinukisha kama kawaida.

“Unapozungumzia Simba ni timu kubwa Afrika sasa na mambo ambayo tunayafanya ni makubwa wapo wale ambao wanataka kutoka kupitia sisi ila hakuna namna ni lazima wakubali kwamba timu yetu ipo imara,” .

Mashindano ya Simba Super Cup yanatarajiwa kuanza Januari 27 ambapo yatashirikisha timu tatu ikiwa ni Simbe yenyewe ambao ni wenyeji, TP Mazembe na Al Hilal.

SOMA NA HII  TETESI...SIMBA SC WAPANIA KUMNG'OA JOB YANGA....MKATABA WATAKAO UMPA HUU HAPA...